MTANGAZAJI

MWENDESHA MASHTAKA AAMURU MCH MACKENZIE NA WENZAKE WASHITAKIWE



Mwendesha mashtaka Mkuu wa Kenya Jumanne ya Januari 16 mwaka huu aliamuru watu 95  wanaotuhumiwa kuongoza Kanisa linalodaiwa kuendesha ibada ya maangamizi washitakiwe kwa mauaji, ukatili, kutesa watoto na uhalifu mwingine katika vifo vya watu 429 wanaoaminika kuwa waumini wa kanisa hilo.

Mkurugenzi wa mashtaka ya umma nchini Kenya , Mulele Ingonga, alikuwa akijibu shinikizo kutoka kwa hakimu katika Kaunti ya Pwani ya Kilifi ambaye aliueleza  upande wa mashtaka kuwafungulia mashtaka washukiwa ndani ya majuma mawili la sivyo mahakama itawaachilia.

Kwa miezi kadhaa tangu kukamatwa kwa watu hao Aprili mwaka jana, waendesha mashtaka walikuwa wameiomba mahakama ruhusa ya kuendelea kumshikilia kiongozi wa kanisa hilo Paul Mackenzie na wengine 28 huku wakichunguza kesi iliyowashtua Wakenya kwa kugunduliwa kwa makaburi ya halaiki na madai ya njaa na kunyongwa.

Hakimu Mkuu Yousuf Shikanda alikataa ombi la hivi punde la kuwashikilia washukiwa hao kwa siku 60 zaidi, akisema upande wa mashtaka umepewa muda wa kutosha kukamilisha upelelezi.

Kesi hiyo iliibuka wakati polisi walipowaokoa waumini 15 waliokuwa wamedhoofika kutoka katika Kanisa la Mackenzie kwenye kaunti ya Kilifi Kusini Mashariki mwa Kenya. Wanne walifariki baada ya kundi hilo kupelekwa hospitalini.
 
Walionusurika waliwaambia wachunguzi kwamba Mchungaji  alikuwa amewaagiza wafunge hadi kufa kabla ya ulimwengu kuisha ili wakutane na Yesu.
 
Upekuzi katika eneo la mbali, lenye misitu ulipata makumi ya makaburi ya watu wengi, mamlaka imesema. Uchunguzi wa maiti kwenye baadhi ya miili ulionyesha njaa, kunyongwa au kukosa hewa.
 
Mashitaka mengine ambayo washukiwa hao watakabiliwa nayo ni pamoja na kuua bila kukusudia, kufanya itikadi kali, shambulio la kudhuru mwili na kujihusisha na uhalifu wa kupangwa.
 
Mackenzie anatumikia kifungo tofauti cha mwaka mmoja jela baada ya kupatikana na hatia ya kuendesha studio ya filamu na kutengeneza filamu bila leseni halali.


 


No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.