MTANGAZAJI

VIONGOZI DINI NA SERIKALI TANZANIA WAMLILIA MUNGU DHIDI YA CORONA (+VIDEO)




Viongozi wa madhehebu mbalimbali ya Dini  nchini Tanzania wameendesha maombi maalum ya kuiombea nchi hiyo  dhidi ya maambukizi ya virusi vya Corona.
Maombi hayo yamefanyika katika Viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam ambapo mgeni rasmi alikuwa ni Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa.
Akizungumza kabla kuanza rasmi kwa maombi hayo, Waziri Mkuu Majaliwa amesema hadi  Aprili 21,2020, Watanzania 284 walithibitika kuambukizwa Corona, 256 wanaendelea vizuri, saba wako chini ya uangalizi, 11 wamepona na kurejea makwao na  watu 10 wamefariki Dunia.
Amesema kuwa Serikali inatambua jitihada kubwa inayofanywa na viongozi wa Dini katika kuhamasisha waumini wao kuzingatia masharti na tahadhari dhidi ya Corona.

Waziri Mkuu ameongeza kuwa ni lazima kuzingatia maelekezo yanayotolewa na wataalam wa afya kwani yatasaidia kuondokana na maambukizi nchini na kupunguza uwezekano wa kuwa na maambukizi mapya ambapo amewataka wazazi na walezi nchini kudhibiti mizunguko isiyo lazima kwa watoto wao ili kukabiliana na maambukizi mapya.
Aidha amezitaka kamati za ulinzi na usalama za mikoa kuzingatia masharti ya kinga dhidi ya ugonjwa huo.
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amekemea tabia ya baadhi ya wafanyabiashara kupandisha bei ya bidhaa ikiwemo Sukari hasa kipindi hiki kuelekea Mwezi Mtukufu wa Ramadhan.
Wakiongoza maombi hayo ya kitaifa baadhi ya viongozi wa dini wamemshukuru Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuruhusu kuabudu na kuliombea taifa dhidi ya janga la Corona nchini. 


Kwa upande wake Mufti wa Tanzania Sheikh Abubakari Zubeir alimwomba yarabi kuondosha mtihani huo wa Coronaamabao umeitikisa dunia kwasasa na kuomba waumini kuendelea kuomba kwajili ya kuondokana na janga hilo.
Naye Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam Jude Thadeus Rwaichi amesema kuwa Mwenyezi Mungu ndiye mlinzi wa Maisha ya mwandamu hivyo ni budi kumuomba yeye ili atupitishe salama na kuondokana na janga hili la Corona.
Viongozi wa Dini walioshiriki maombi hayo ni kutoka Madhehebu ya  Roman Katoliki,Kiislamu, Jumuiya ya Kikristo Tanzania, Jumuiya ya Mabohora, Kanisa la Pentekoste, Kanisa la Waadventista wa Sabato, Mwakilishi wa Mufti wa Zanzibar na wafuasi wa madhebu ya Budha Tanzania.
Maombi haya dhidi ya maambukizi ya homa kali ya mapafu inayoambukizwa na virusi vya Corona ni mwendelezo wa maombi ya kitaifa yaliyoitishwa na Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kuanzia Aprili 17 hadi 19, 2020 kote nchini Tanzania.
Mapema Aprili 9, 2020 Viongozi wa Dini na baadhi ya Viongozi wa Serikali walikutana jijini na Dar es Salaam na kuazimia kufanyika kwa maombi maalum ya kitaifa yanayoshirikisha waumini wa madhebu yote nchini Tanzania ili kuiombea nchi dhidi ya maambukizi ya virusi vya Corona.

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.