MTANGAZAJI

MIUNDOMBINU YA KITUO CHA FORODHA CHA HOROHORO HAIKIDHI VIWANGO-SERIKALI


Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) (kushoto) na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe.  Damas Ndumbaro (kulia), wakihoji namna ambavyo Kituo cha pamoja cha Forodha - Horohoro  kinavyotunza kumbukumbu za vyombo vya moto vinavyoingia na kutoka,Katikati ni Afisa Mfawidhi wa Uhamiaji  Kituo cha pamoja cha Forodha - Horohoro Bw. Antony Kasitu. 
Serikali ya Tanzania  imetoa agizo kwa watendaji wa Kituo cha pamoja cha Forodha Mpakani- Horohoro, kuwasilisha nyaraka za ujenzi wa Kituo hicho ukiwemo mkataba, kwa kuwa miundombinu iliyopo haijakidhi viwango jambo lililosababisha kutofunguliwa rasmi kwa kituo hicho tangu mwaka 2015.

Agizo hilo limetolewa na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango nchini Tanzania Dkt. Ashatu Kijaji na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt. Damas Ndumbaro walipofanya ziara ya kutembelea na kukagua Kituo hicho ambapo hawakuridhishwa na miundombinu yake.

Dkt. Kijaji, alisema kuwa Kituo hicho hakina mawasiliano kati ya upande wa Tanzania na Kenya hivyo kutokidhi vigezo vya kuwa Kituo cha pamoja cha Forodha kati ya nchi hizo mbili.

Alisema kuwa ukosefu wa mawasiliano unasababisha urasimu katika kuwahudumia wananchi jambo linalosababisha wateja katika mpaka huo kutafuta njia nyingine ambazo sio rasmi katika usafirishaji bidhaa jambo ambalo linaathari kubwa katika ukusanyaji wa mapato.

Miongoni mwa kasoro zilizobainika wazi ni kamera maalum za usalama zinazotakiwa kufanyakazi ni zaidi ya 14 lakini zinazofanyakazi mpaka sasa ni 4 pekee jambo linalotiashaka kuhusu usalama wa Kituo hicho

Dkt. Kijaji, alisema pia, utaratibu wa wakazi wa Horohoro kwenda kupata huduma za TRA katika Wilayani Muheza usitishwe na badala yake watumishi wa Mamlaka hiyo waende kuwahudumia wananchi katika Wilaya ya Mkinga ili kuondoa usumbufu kwa wafanyabiashara wanapotaka kulipa kodi au kutafuta huduma za masuala ya forodha.

Aidha, Manaibu Waziri hao wameiagiza Mamlaka ya Mapato (TRA) Mkoani Tanga kuhakikisha Jenereta la Kituo hicho cha Pamoja cha Forodha linafanyakazi ndani ya saa 24 ili kukabiliana na upotevu wa mapato katika eneo hilo kinyume na hapo hatua zingine zitachukuliwa.

Manaibu Waziri hao wametoa maagizo hayo baada ya kuelezwa kuwa jenereta halifanyikazi baada ya kuharibika kwa takribani siku 14 na kusababisha Seikali ikose mapato na kuleta usumbufu kwa watumiaji wa Kituo hicho kwani hulazimika kukaa muda mrefu kusubiri umeme urejee baada ya kukatika.

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.