MTANGAZAJI

ASILIMIA 80 YA WAKAZI WA MWANZA HAWANA VYOO BORA

Wakati serikali ya Tanzania ikiwa imetiliana saini Mkataba na Benki ya Kitega uchumi ya Umoja wa Ulaya(EIB)na Shirika la Maendeleo la Ufaransa(AFD)ili kutekeleza Mradi wa Maji safi na Mazingira ya Jiji la Mwanza,utafiti unaonesha kuwa zaidi ya asilimia 80 ya wakazi wa Mwanza hawana vyoo bora,na hutiririsha maji taka kikiwemo kinyesi katika ziwa Victoria ambapo asilimia  85 ya wakazi wa jiji hilo hawajaunganisha maji taka yao katika mfumo wa maji taka ulioko Butuja.
 
Mkataba huo umesainiwa Machi 5 mwaka huu, kwa lengo la kuongeza upatikanaji wa maji ya kunywa kwa wakazi wa Jiji la Mwanza,hususan katika maeneo ambayo hadi sasa hulazimika kunywa maji ya visima,kwa kuwa hayafikiwi na maji ya bomba.
 
 Mradi huo utawezesha usafi wa mazingira kwa wakazi wa milimani katika jiji hilo,ikiwa ni pamoja na kujenga vyoo katika shule za msingi ambazo wanafunzi zaidi ya 100 hulazimika kutumia tundu moja la choo kwa siku.
 
 
Mkurugenzi wa Maji Safi na Maji Taka jijini Mwanza,MWAUWASA,Mhandisi Anthony Sanga, ameiambia amewaambia waandishi wa habari leo kwamba, mradi huo mkubwa wa matangi makubwa,utaongeza maji kwa kiasi cha mita za ujazo 50,000 kwa siku.
 
Kulingana na Mhandisi huyo wa MWAUWASA,Anthony Sanga,mradi huo ukikamilika utaondoa kero ya maji kwa wakazi wa maeneo ya Buswelu,Kiseke,Ibanda,Kabuhoro,Kirumba na maeneo mengine ya jiji ambako akina mama hulazimika kudamka usiku wa manane kutafuta maji.

  Zaidi ya Euro milioni 104.5 sawa za shilingi za Tanzania Bilioni 219.5 zimetengwa kutekeleza mradi huo, ambazo zitatolewa na wafadhili hao,wakati serikali ya Tanzania itachangia kiasi cha Euro Milioni 14.5,sawa na shilingi za Tanzania bilioni 30.5
 
Kulingana na MWAUWASA,Mradi huo wa usafi jijini Mwanza ni utekelezaji wa Matokeo Makubwa sasa(BRN),na lengo ni kuondoa tatizo la maji salama na uchafuzi mkubwa wa mazingira unaofanywa na wakazi wa milimani.
 
Na:Conges Mramba

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.