BARAZA LA MADIWANI TARIME LATAKA WAZAZI WASIOPELEKA WATOTO SHULE WASHITAKIWE
Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya
Wilaya ya Tarime limepitisha azimio la kuwafikisha mahakamani wazazi ambao
hawawajibiki ipasavyo kuwapeleka watoto waliofaulu kujiunga kidato cha kwanza
mwaka huu ili kujibu tuhuma za kutotekeleza jukumu hilo baada ya wakuu wa shule
za sekondari kuyabaini majina ya wanafunzi watoro.
Azimio hilo limefikiwa katika kikao
cha baraza la madiwani kinachofanyika kwenye ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya
Tarime ambapo wamemtaka Mkurugenzi Mtendaji Athuman Akalama kushughulikia
tatizo hilo haraka ili kuboresha kiwango cha elimu kinachoelezwa kushuka
wilayani humo.
Diwani wa kata ya Pemba Paradiso
Mogesi amesema kuwa katika kata yake asilimia 21 ya wanafunzi waliochaguliwa
kujiunga na kidato cha kwanza kwa mwaka 2014 hawajaripoti kwenye shule
walizopangiwa kujiunga.
Amesema kuwa ili kukomesha tabia
hiyo ya baadhi ya wazazi wasioona umuhimu wa kuwapeleka watoto wao shule katika
vikao toka ngazi ya vijiji na mkutano mkuu wa kata, wamewaagiza wakuu wa shule
za sekondari katika kata yake kuwaorodhesha wanafunzi wote ili kubaini
wanafunzi watoro na kuanza kuwashughulikia wazazi wao.
Afisa utumishi wa Halmashauri hiyo
Bakaran Urio akionesha kuguswa na hali hiyo amewataka viongozi husika kulifikisha tatizo hilo ofisini kwake
ili kulishughulikia haraka iwezekanavyo.
Post a Comment