MTANGAZAJI

VITAMBULISHO VYA TAIFA NCHINI TANZANIA KUANZA KUTOLEWA FEBRUARI 7,2013


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete akitia saini ya kitambusho cha Taifa
Mamlaka  ya Vitambulisho vya Taifa nchini (NIDA) imemweleza Rais Jakaya Kikwete kuwa Vitambulisho vya Taifa vinatarajia kuanza kutolewa rasmi Februari 7, 2013. Taarifa hiyo imetolewa jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), Dickson Maimu wakati Mkurugenzi huyo na ujumbe wake walipofika nyumbani kwa rais kukamilisha taratibu za uandikishaji wa kitambulisho chake.

Kwenye tukio hilo la muda mfupi na lililoshuhudiwa pia na Mama Salma Kikwete, Rais Kikwete ametakiwa kuthibitisha ukweli wa habari zilizojazwa kwenye fomu yake ya uandikishaji, akapiga picha rasmi ya kitambulisho chake na kutiwa saini kwenye kitambulisho chake anachondaliwa na NIDA.

Maimu amemwambia Rais Kikwete kuwa wakati wa uzinduzi huo wa utoaji Vitambulisho vya Taifa utakaofanyika kwenye Viwanja vya Karimjee, Dar es Salaam, NIDA itatoa vitambulisho kwa viongozi wakuu wa taifa na viongozi wakuu wastaafu.

Amesema kuwa baada ya sherehe hizo ya uzinduzi wa utoaji Vitambulisho vya Taifa, maofisa wa NIDA watatoa Vitambulisho kwa Wabunge na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar. Maimu pia amemwambia Rais Kikwete kuwa inakadiriwa kuwa kiasi cha Watanzania milioni 21, wenye umri wa zaidi ya miaka 18, watajiandikisha kwa ajili ya kupatiwa Vitambulisho na kuwa orodha hiyo itaweza kutumiwa na taasisi nyingine nchini ikiwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi na mabenki.

Rais Kikwete pia alitaka kujua nchi nyingine zinaendesha vipi suala zima la vitambulisho hasa kuhusiana na kuvitoa bure kwa wananchi na Maimu amesema kuwa kwa Tanzania gharama za Vitambulisho vya Taifa zitabebwa na taasisi ambazo zitatumia habari na takwimu zilizoandaliwa na NIDA.
Rais Kikwete ameishukuru mno NIDA kwa hatua zilizofikia kuelekea kupatikana kwa Vitambulicho vya Taifa. “Nawashukuru sana kwa kufikia hatua ya sasa. Tumeanza mbali mno na suala hilo, tokea mwaka 1968. Nafurahi sana kuwa tumefikia mahali pa kuweza kutoa Vitambulisho vya Taifa.”

NIDA ilianza zoezi la kuandikisha wananchi kwa ajili ya kutoa Vitambulivyo vya Taifa mwishoni mwa mwaka 2011 baada ya kukamilisha zoezi zima la maandalizi ya kuifanya kazi hiyo.
Chanzo:The Habari.com

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.