MTANGAZAJI

FURSA ZA TEKNOHAMA KWA VIJANA

 

 Serikali  imewahimiza vijana wa Tanzania kutumia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEKNOHAMA) kukamata fursa zilizopo nchini katika Sekta ya Mawasiliano.

Hayo yameelezwa na Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari nchini humo, Mulembwa Munaku wakati akifungua Kongamano la Kidijitali la Vijana Tanzania kwa niaba ya Waziri wa Wizara hiyo, Dkt. Faustine Ndugulile lililofanyika Dar es Salaam.

Munaku amesema kuwa Serikali imeweka mazingira wezeshi na rafiki ya
kuendeleza na kufanikisha matumizi ya TEKNOHAMA nchini ambapo Wizara hiyo imetengeneza sera ya Taifa ya TEKNOHAMA; sheria na kanuni; ujenzi wa miundombinu ya TEHAMA ikiwemo Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano wenye urefu wa kilomita 8,319 unaofikisha huduma za mawasiliano kwenye mikoa na nchi jirani.

Ameongeza kuwa zaidi ya asilimia 75 ya watanzania ni vijana ambapo Serikali
imetambua hilo hivyo imeweka mikakati na miradi ya TEKNOHAMA inayogusa vijana ili kuongeza wigo wa fursa za TEKNOHAMA kwa vijana katika nyanja mbali mbali ikiwemo fursa ya ajira; biashara; mafunzo; na ubunifu ili TEKNOHAMA itumike kutatua na kujibu changamoto zilizopo kwenye jamii.

Amefafanua kuwa katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2021, Serikali
imepata mkopo nafuu wa dola za kimarekani milioni 150 kutoka Benki ya Dunia ili kutekeleza mradi wa Tanzania ya Kidijitali ambapo mradi huo utagusa vijana na TEHAMA katika nyanja ya kiuchumi na kijamii.

Naibu Kiongozi wa Ujumbe wa Umoja wa Ulaya nchini Tanzania, Emilio Rossetti
amesema kuwa kupitia umoja wao wamekuwa wakitoa misaada nchini na kushirikiana na Serikali kuendeleza na kuongeza matumizi ya TEHAMA nchini
hususan kwa vijana na wanawake na wako tayari kuendelea kufanya hivyo ili vijana wanufaike na fursa za TEKNOHAMA zilizopo.

Naye Mkurugenzi Mkazi wa Kampuni ya DOT Tanzania, Diana Ninsiima amesema kuwa kampuni hiyo imeshirikiana na wadau wengine kuandaa Kongamano hilo ili litumike kama jukwaa la kujenga uelewa kwa jamii kuhusu nafasi ya vijana katika TEKNOHAMA ambapo kauli mbiu ya mwaka huu ni, “Ujuzi wa Kidijitali kwa ajili ya Ajira na Ujasiriamali kwa Vijana,”.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Mtabe Innovations, Given Edward,
akizungumza kwa niaba ya vijana wenzake amesema kuwa hivi sasa vijana wa
kitanzania wanapata mazingira sawa na vijana wengine duniani kutumia TEHAMA kuendesha maisha yao na wanaishukuru Serikali kwa kubadilisha mitazamo ya jamii kuhusu umuhimu na manufaa ya TENOHAMA kwa vijana na kuongeza ushiriki wa vijana katika TEKNOHAMA.

Kongamano hilo limehudhuriwa na wadau mbali mbali waliokuwepo ukumbini na wengine kwa njia ya mtandao wakiwemo kutoka Umoja wa Mawasiliano Duniani; Ofisi za ubalozi wa Canada, Ireland; UNICEF; Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia; Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia; na kampuni za TEKNOHAMA za vijana zilizopo nchini Tanzania.

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.