MTANGAZAJI

BOMU LALIPUKA KWENYE NYUMBA YA KANISA


Mhudumu wa nyumba ya kupumzikia wageni wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Mashariki ya Ziwa Victoria, jijijini Mwanza, amejeruhiwa baada ya kulipukiwa na bomu lililokuwa limewekwa kwenye kiambaza cha nyumba hiyo.

Tukio hilo lilitokea juzi kati ya saa 1:45 na saa 2:20 usiku, katika eneo la Makongoro wilayani Ilemela wakati mhudumu huyo, Bernadetha  Alfred (25), alipofungua kifurushi cha mzigo alichodhani kimesahaulika kwenye eneo hilo, kabla ya kumlipukia.

Kwa mujibu wa Katibu wa Dayosisi hiyo, Mollel Rogart, kifurushi hicho kilichokuwa kwenye mfuko mweusi wa nailoni, kilikuwa juu ya kreti tupu za soda kwa muda wa siku tatu, karibu na eneo la kulia chakula lililopo katika nyumba hiyo.

 Kamanda wa polisi mkoani Mwanza, Valentino Mlowola, akithibitisha kutokea kwa tukio hilo jana na kusema kwamba uchunguzi wa awali uliofanywa na kikosi maalum kutoka Dar es Salaam umebaini kuwa bomu hilo limetengenezwa kienyeji.


Mlowola alieleza kuwa, Bernadetha aliyejeruhiwa katika sehemu mbalimbali za mwili, alikimbizwa katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando ambako anaendelea na matibabu.

Kamanda huyo alieleza kwamba, mabomu (yakiwemo ya kienyeji) yako katika mifumo mbalimbali, hivyo wananchi hususan wahudumu wa sehemu za mikusanyiko wawe na tahadhari na vitu vinavyoonekana kusahaulika na wasisite kuwajulisha polisi vinapoonekana.

Mlipuko huo uliozusha hofu kwa waumini mbalimbali wakiwamo wa kanisa hilo, umetokea ikiwa ni juma moja baada ya maadhimisho ya ‘Huduma ya Mtoto’ kwa makanisa mbalimbali ya Kikristo jijini Mwanza yaliyofanyika kwenye kanisa hilo. 


No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.