MTANGAZAJI

MWAKA MMOJA JELA KWA KOSA LA KUMSHAMBULIA MKEWE KWA PANGA NA FIMBO

Amosi Samwel Nkororo akiingia kwenye gari la polisi amefungwa pingu kwenda kutumikia kifungo cha mwaka mmoja jela(Picha na WaitaraMeng’anyi)
Amosi Samwel Nkororo 38 mkazi wa kijiji cha Sirari kata ya Sirari  tarafa ya Inchugu Wilaya ya Tarime amehukumiwa mwaka mmoja jela kwa kosa la kumshambulia mkewe kwa panga na fimbo na kumsababishia majeraha kichwani Wilayani hapa.

Aliutenda unyama huo juni moja saa 11  jioni alipoingia nyumbani na kuanza kumshabulia mkewe aitwaye Mariam Daniel 34 kwa panga akimtuhum u kulala nje ya familia bila taarifa ama ruhusa yake.

“Nilipigiwa simu jana  yake siku ya tarehe 31 kuwa mama mzazi anaumwa nikaamua kukimbia kwenda kumwaona kwa kuwa ni mtu mzima huko Magoto, nililala na kesho yake saa tatu asubuhi nilikuwa kwangu maana niliwaacha watoto wadogo” alisema Mariamu.

Mariamu Daniel miaka 34 aliondoka na kuripoti kituo cha polisi sirari  na kupewa kibali  cha kutibiwa akiwa amekimbia mji kwa kuwa Nkororo alikuwa akimtafuta  kwa kile kilichodaiwa kuwa alitaka kumwondoa uhai huku akidai kuwa muke hawezi kumiliki hati ya Nyumba waliojenga

Mariamu ameeleza kuwa wameishi pamoja kwa muda wa miaka mitano na  katika muda huo walikuwa wakiishi vizuri  japo Nkororo  alikuwa akimfanyia  ukatili kwa kumpiga jambo ambalo alilichukulia kuwa ni la kawaida.

Baada ya kuona hali ya maisha ya mumewe si nzuri kwa kuwa ni msukuma toroli Mariamu aliamua kwenda kwenye kikundi kukopa  shilingi laki tano  kumletea mumewe aweze kuwa anachukuwa machungwa kutoka Musoma na kuyauza  ili  kuongeza kipato katika familia yao, huku akimpa  shilingi elfu 20 kila mwezi kurudisha katika kikundi chake.

Mariamu ameeleza kuwa fedha hizo zilitumika kwa starehe na hazikuleta faida yoyote zaida ya kuwa analeta wanawake nyumbani huku akinoa panga na kisu  akimtishia kuwa atamchinja kwani yeye ni mtu kuja akimaanisha si mzaliwa wa Sirari.

“Shida ilianza baada ya kununua uwanja na kuanza kujenga hii nyumba alianza kuniambia nimpe barua ya mkataba wa kununulia ploti hii, na alipoona sifanyi anavyotaka akaanza kujaribu kujinyonga nyakati za usiku wakati Fulani akichora ramani ya kaburi hapo uani akisema hapa ndipo nitakapo zikwa nikifa” alisema . Mariamu Daniel.

Kutokana na kipigo hicho cha mwezi juni mariamu aliamua kwenda kwa sheria  kutafuta usaidizi. Chini ya mwongozo wa kituo cha SHEHABITA  aliifikisha kesi hiyo mahakama ya mwanzo ya Sirari na kuamua kuisimamia  kwa kipindi chote cha miezi sita.

Hata hivyo Bi Mariamu anaonekana msaliti wa mila na desturi kwa kumshitaki mumewe na kuhukumiwa kifungo cha mwaka mmoja.

“Wanawake wenzangu wananishangaa wananiuliza hivi kweli umemfunga mume wako si utaharibu mahusiano yako na wakwe zako?” alieleza

Hata hiyo wakazi na mashuhuda wa hukumu hiyo ambayo ni ya kwanza kufikia hukumu wamshukuru bi Mariam kuwa jasiri na kusimamia kesi yake hadi mwisho maana waengi huzifungua kesi za namna hiyo na baadaye kutoroka hazijafikia hukumu.

“sikutumia hata senti moja katika kesi hii bali ni maelezo yangu na ushahidi wa mwanagu Shadrack Mwita 10 alioutoa nimetendewa haki japo adhabu aliyopewa bado mimi naona ni ndogo kutokana na maumivu aliyonisababishia kichwani” alisema .

Akisoma hukumu  katika mahakama ya mwanzo Sirari Hakimu Bi, Pestaflora Chacha alieleza kuwa mnamo tarehe moja ya mwezi wa sita mwaka Nkororo alimshambulia mkewe kwa panga kwa kumkata majeraha mawili kichwani na kumsababishia maumivu makali yaliyomsababisha kulazwa na kushonwa nyuzi 8 kwa jeraha la kwanza na  nyuzi 6 kwa jeraha la pili.

Nkororo aliiomba mahakama ipunguzie adhabu kwa kuwa anategemewa na familia na kubadilishiwa adhabu ili apewe kifungo cha nje angalau cha kufagia na kufanya usafi eneo la mahakama hiyo ya mwamzo.

“Adhabu uliyopewa ni ndogo kulingana na kosa ulilolifanya, na ni kwa kuwa Mahakama hii ina uwezo wa kutoa  adhabu ya kiwango hicho hata hivyo nakutuma mahakama ya Wilaya ili hukumu yako ipitiwe ikionekana nimekuonea watakupunguzia na ikionekana nimekuhurumia itajuwa cha kufanya” alisema Hakimu Bi, Pestaflora.

Hata hivyo Hakimu Pestaflora akitoa hukumu hiyo amesema, kutokana na kitendo cha Nkororo kumshambulia mkewe kwa kudai kuwa alikuwa akimrudi  ambacho ni kinyume cha sheria ya ndoa namba 5 ya mwaka 1971 kifungu cha 66 kinachosema  si mume wala mke atakayerusiwa kumpiga mwenzake kwa kosa liwalo lote amemhukumu kifungo cha mwaka mmoja jela kulingana kiwango cha adhabu inayoruhusiwa kisheria kutolewa na mahakama ya mwanzo japo alistahili adhabu kubwa zaidi.

Aidha ametoa hukumu hiyo kuwa fundisho kwa wanaume wengine wenye tabia  mfumo dume waitumiayo kutatua migogoro ya familia zao ambayo imepitwa na wakati.

Naye Mkurugenzi wa chama cha  waandishi wanawake Tanzania TAMWA Bi Valerie Msoka ameishukuru mahakama kwa kumtendea haki Bi Mariamu kwa kumhukumu mumewe kutokana na ukatili aliounesha kwake, aidha ametoa rai kwa mahakama vyesi vya ukatili vichukue muda mfupi kusikilizwa na kutolewa hukumu badala ya kuchukuwa muda mrefu ili kuwafanya wakatiliwa kupata haki yao ya kisheria kwa wakati.

“Tunawaomba wanawake wote wanaofanyiwa unyanyasaji huu popote wakaripoti katika vituo vya polisi na kupeleka kesi hizi mahakamani kwani haki inatendwa wazisimamie  hadi mwisho wasiogope” alisema mkurugenzi huyo wa TAMWA.

Naye msaidizi wa sheria na haki za bindamu Bwn, Mrimi Zabroni ameelea kufurahishwa kutokana na maamuzi yaliyofikiwa na mahakama hiyo katika shauri namba 169 la mwaka 2013 kufikia hukumu.

“Hii ni kesi ya kwanza kutolewa hukumu tangu nianze kazi na imenitia moyo kuendelea kuwasaidia wanaoonewa kwa kuwaonesha wapi haki yao ilipo kwa kufuata sheria kwani sheria zipo na zinztekelezwa kwa kufuta misingi ya nchi” alisema Zabron msaidizi wa sheria kutoka shirika la haki za binadamu SHEHABITA
Imeandikwa na Waitara Meng'anyi toka Tarime

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.