MTANGAZAJI

KANUNI NA SHERIA ZA VYOMBO VYA HABARI TANZANIA

Waziri anayesimamia Sekta ya Habari nchini Tanzania Innocent Bashungwa na Waziri anayesimamia Sekta ya Mawasiliano Dkt. Faustine Ndugulile na timu ya Makatibu  Wakuu na Wataalam  wa Wizara hizo  wamekaa na kujadili  hoja mbalimbali kuhusu  utekelezaji wa Sera, Sheria na Kanuni za kisekta kufuatia  maelekezo  ya hivi karibuni ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.


Majadiliano hayo yamefanyika jijini Dodoma Aprili 14, 2021 na kutoa mapendekezo ya hatua za kuchukuliwa kwenye hoja 13 zilizoainishwa na Wizara hizo kufuatia wakati wa  kuwaapisha Makatibu Wakuu, Naibu  Makatibu  Wakuu na  Wakuu wa Taasisi ya kufanya  marekebisho ya Sheria na Kanuni  zinazosimamia Vyombo vya Habari hususan Televisheni Mtandao (Online TV).


Miongoni mwa  maazimio  yaliyofikiwa ni pamoja na kufanya  mapitio ya Sera, Sheria,Kanuni na Miongozo katika maeneo yote yenye mapungufu  ili ziendane na  hali halisi ya sasa  na  kuweka  mifumo rafiki ya kushughulikia masuala  yote  yanayohusu sekta ya  Mawasiliano na Utangazaji.


Pia, Wizara zimeaazimia kuja na mkakati wa kuwaelimisha  wadau wa Sekta hizo ili kudhibiti makosa  ya kimaudhui  yanayofanywa  na Vyombo vya Habari badala ya hali ilivyo sasa inayotoa adhabu kali zinazojikita kwenye utozaji wa faini kubwa pamoja na kufungiwa.


Suala lingine ambalo limeazimiwa kufanyiwa kazi ni chaneli za bure kutoonekana kwenye visimbusi ambavyo kimsingi zinapaswa kuonekana hata pale kifurushi kinapokuwa kimeisha muda wake.

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.