DAR ES SALAAM:MAAMUZI ALIYOYAAGIZA RAIS WA TANZANIA DR MAGUFULI LEO YAKO HAPA
Rais wa Tanzania Dr John Pombe Joseph Magufuli katika kikao na watendaji wa serikali leo ikulu jijini Dar es salaam |
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Drt.John Pombe Joseph Magufuli amefuta safari zote za nje za watendaji wakuu wa serikali huku zile zenye ulazima zikitakiwa kutolewa kibali maalum na Rais ama Katibu Mkuu Kiongozi ambapo pia ameawataka watendaji hao wakuu wa serikali kufanya ziara za vijijini ili kujionea kero za wananchi na kuweka mikakati ya kuzitatua.
Rais Drt.John Pombe Magufuli akiwa na makamu wake wa Rais ametoa
maagizo hayo katika mkutano wake alioufanya na watendaji wakuu wa
serikali wakiwemo makatibu wakuu na Manaibu wao,Gavana wa Benki kuu
pamoja na Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania( TRA).
Katika mkutano huo Rais Dr .Magufuli amewataka watendaji hao
kuwaachia mabalozi wa Tanzania walioko katika nchi mbalimbali
kushughulikia shughuli zote zinazopaswa kufanywa nje ya nchi mpaka hapo
atakaposema vinginevyo.
Aidha amemtaka Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA)
Rished Bade kusimamia kikamilifu na kwa uadilifu suala la ukusanyaji wa
mapato hasa kwa wafanyabiashara wakubwa na wale wanaokwepa kodi bila ya
woga wala uonevu ili kuiwezesha serikali kuwa na fedha zitakazowezesha
kutatua kero za wananchi kama alivyoahidi katika kampeni zake.
Aidha rais Dr.Magufuli pia ameagiza usimamizi makini na uadilifu
katika manunuzi ya serikali ambayo yamekuwa yakitumiwa vibaya na kutoa
mwanya kuibia serikali kwa kuongeza bei hata kama bidhaa yenyewe ni ya
bei ya chini na kwamba watendaji watakaobainika kufanya ujanja ujanja
ama ubadhirifu katika manunuzi watawajibishwa mara moja.
Pia Rais Dr.Magufuli ameagiza utekelezwaji wa utoaji wa elimu bure
kuanzia darasa la kwanza hadi kidato cha nne kuanzia mapema mwakani na
kuagiza suala la mikopo ya wanafunzi wa elimu ya vyuo vikuu lifanyiwe
kazi na mipango yake kwa ajili ya utekelezaji ili kuwaondolea kero
wanafunzi.
Post a Comment