MTANGAZAJI

DODOMA:SHEREHE ZA KUKABIDHI KATIBA ILIYOPENDEKEZWA KUFANYIKA KESHO



Sherehe za kukabidhi Katiba inayopendekezwa kwa Rais Jakaya Kikwete na Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein itafanyika kesho kwenye uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma.

 Sherehe  hiyo  itakayoanza saa 6:00 mchana itahudhuriwa na  marais wastaafu wa Zanzibar na Tanzania Bara,mabalozi wanaoziwakilisha nchi zao nchini , viongozi wa ngazi tofauti wa kitaifa, watu mashuhuri na wawakilishi wa makundi yote ya jamii ya Watanzania, ambayo yameguswa na katiba hiyo inayopendekezwa.

Oktoba 2 mwaka huu Bunge maalumu la Katiba nchini Tanzania lilipitisha rasimu ya katiba iliyopendekezwa,hatua hiyo ilifikiwa baada ya kura za ndio zilizopigwa na wajumbe kufikia kiwango kinachostahili, ili katiba hiyo iliyopendekezwa ipite ilitakiwa kuungwa mkono na kura za ndio theluthi mbili kutoka Tanzania bara na theluthi mbili za ndio kutoka Zanzibar.

Jumla ya wajumbe wote wa bunge hilo la Katiba ni 629, huku 419 wakitoka Tanzania bara na 210 kutoka Zanzibar.

Zoezi hilo la upigaji kura ambalo lilianza Septemba 29 mpaka Oktoba 2, siku matokeo yalipotangazwa, lilisusiwa na wabunge wengi wa upinzani, kwa madai kuwa baadhi ya vipengele vya awali vilivyopendekezwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliyopewa kazi ya kukusanya maoni kutoka kwa mwananchi, vilikuwa vimeondolewa.

Rasimu hiyo ya katiba ilipendekezwa na kamati ya uandishi kuwa na jina la KATIBA YA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA YA MWAKA 2014 .

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.