MTANGAZAJI

SERIKALI YAITAKA POSTA KUTOA HUDUMA ZENYE TIJA

 


 
 Makamu wa Rais Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Isdor Mpango amesema , Serikali inahitaji kuona utendaji wenye tija wa Shirika la Posta ikiwa ni pamoja na kuwahudumia wananchi kwa ufanisi kupitia mtandao mpana wa Shirika la hilo lenye matawi zaidi ya 350 yaliyosambaa nchi nzima, bara na visiwani.
 
 Dkt. Philip Isdor Mpango amesema Serikali inafurahi uwepo wa uhusiano mkubwa kati ya malengo makuu ya Umoja wa Posta Duniani na malengo ya Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025 na yale ya Sera ya Taifa ya Posta ya 2003 hasa katika kuwahudumia wananchi.

Makamu wa Rais  Dkt. Mpango alikuwa Mgeni rasmi  wakati wa kuhitimisha siku ya Posta duniani katika maadhimisho ya siku hiyo yaliyofanyika ukumbi wa Jakaya Kikwete jijini Dodoma.

Akiwahutubia mamia ya wakazi wa mkoa wa Dodoma, wageni kutoka sehemu mbalimbali na watoa huduma washiriki wa huduma za mawasiliano nchini, Dkt. Mpango amesema Serikali ya Tanzania  imeshuhudia mageuzi makubwa ndani ya Shirika la Posta, kutokana na huduma mbalimbali zilizoanzishwa na shirika hilo zikiakisi matumizi ya Teknolojia katika kuwahudumia watanzania.

“Tumeshuhudia Posta ikibadilisha namna ya utoaji huduma zake kwa jamii kulingana na mahitaji na ndio maana leo hii tunashudia hatua ya Posta kuwa ya kidigitali na kuweza kuwafikia watu wengi kwa urahisi zaidi “ alisema Makamu wa Rais Dkt. Mpango.
 
“Ni muhimu taasisi hii iguse jamii kihuduma kwakuwa ilianzishwa ili kuhakikisha inatoa huduma kwa niaba ya Serikali na kuwahudumia wananchi wote bila kujali mahali walipo – Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania”.

Kwa upande wake Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dkt. Ashatu Kijaji amesema Wizara yake imefanya maadhimisho hayo kwa siku nne mfululizo na kushirikisha wadau mbalimbali katika Sekta ya Posta na nje ya Sekta ya Posta, nia ikiwa ni kuonesha Umma umuhimu wa huduma za Posta nchini.

Awali akizungumza katika kilele cha maadhimisho hayo ya siku ya Posta Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi, kutoka Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Rahma Kassim Ali amesema serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inatoa hongera kwa umoja wa Posta duniani kwa kufikisha miaka 147 tangu kuanzishwa kwake akisema siku ya Posta duniani inabeba dhana muhimu sana ya Muungano.

“ Hata kama hatuongei lugha moja lakini dunia nzima inaunganishwa na nguvu ya barua na mizigo inayowekwa stempu” alisema, Rahma Kassim Ali.
Katibu Mkuu Mtendaji wa Umoja wa Posta Afrika (PAPU), 
 
Ndg. Sifundo Chief Moyo ambaye pia ameshiriki katika kilele cha maadhimisho hayo amesama PAPU itaendelea kushirikiana na nchi mwanachama za umoja huo katika kusambaza taarifa na miongozo pamoja na kufanya tafiti mbalimbali, akisisitiza kuwa dunia haina budi kujifunza kutokana na Janga la UVIKO-19 na majanga mengine kubadilika kulingana na mazingira ili kuweza kuendelea kumudu utoaji huduma kwa wateja .

Kila Ifikapo Oktoba 9 ya kila mwaka, Tanzania kama mwanachama wa Posta duniani aliyejiunga mwaka 1963, huungana na nchi nyingine duniani kuadhimisha siku ya umoja huo ulianzishwa mwaka 1874.

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.