MTANGAZAJI

VITA DHIDI YA UKATILI IANZIE NGAZI YA FAMILIA

 


Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii, Dkt. John Jingu  amesema zinahitajika mbinu shirikishi kuanzia ngazi ya Familia za kukabiliana na vitendo vya ukatili ikiwemo mimba za utotoni.

Dkt. Jingu ameyasema hayo Jijini Dodoma katika kikao chake na Wajumbe wa Mtandao wa kutokomeza Ndoa za Utotoni Tanzania TECMN ikiwa ni njia ya kupambana na vitendo vya ukatili.

Amesema mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia zikiwemo ndoa za utotoni yanatakiwa kuanza katika ngazi ya familia na hatimaye mifumo yake kuendelea hadi taifa.

Akitoa mifano katika baadhi ya mikoa, Katibu Mkuu Jingu amesema pamoja na jitihada zinazochukuliwa na serikali katika kusimamia sheria za kuharamisha vitendo hivyo, bado vitendo hivyo vinaendelea kutokana na mila na desturi za jamii husika.

Amesema baadhi ya ndugu na wanafamilia wanachelea kutoa ushahidi wa unyanyasaji kutokana na ukali wa sheria zilizopo ili kuwanusuru wanafamilia wanaohusika katika vitendo hivyo vya ukatili ikiwa ni pamoja na kuwakatili watoto kwa kuwapa mimba.

Akizungumzia njia za mapambano dhidi ya ukatili huo, Katibu Mkuu amesema mkakati wa kuboresha uchumi wa kaya kwa kuwawezesha wanawake kushiriki katika uzalishaji mazao ya kimkakati hivyo kuimarika kiuchumi na kushiriki kuzitunza familia zao.

Ameshauri kampeni za kukomesha ukatili zifanyike kwa kushirikisha vyombo vya habari na watu wenye ushawishi katika jamii husika wakiwemo viongozi wa dini ili kuwezesha jamii kutambua tatizo na kuchukua hatua za kulikataa.

Amefafanua kuwa kuna hatua zilizochukuliwa kupitia Mpango kazi wa taifa wa kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake na watoto MTAKUWWA kuanzia ngazi za chini lakini bado jitihada zaidi zinahitajika kuhakikisha kamati hizo zinafanya kazi kwa ufanisi.

Ameongeza kuwa ni muhimu kuwa na vituo vya malezi na makuzi ya awali ya watoto katika jamii ili waweze kujihusisha na mambo yanayoweza kuwakuza kiakili badala ya kuachwa bila uangalizi na hatimaye kujikuta katika mazingira hatarishi.

Mtandao wa TECMN unajumuisha Mashirika 64 Yasiyo ya kiserikali ambao unafanya kazi katika ngazi ya kitaifa na kikanda.  


No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.