MTANGAZAJI

NAIBU WAZIRI MWANAIDI ATAKA ULINZI KWA WANAWAKE NA WATOTO DHIDI YA VITENDO VYA UKATILI

 


Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto,Mwanaidi Ali Khamis amewataka watendaji wanaosimamia utekelezaji wa Sheria ya ulinzi wa haki za wanawake na watoto dhidi ya vitendo vya ukatili kuhakikisha haki inapatikana ndani ya kipindi kilichowekwa na ikiwezekana ipatikane kwa haraka zaidi.
Naibu Waziri Mwanaidi amesema hayo, Wilayani Kasulu mkoani Kigoma alipofika katika nyumba moja ya kuwahifadhi wanawake na watoto waliokumbana na vitendo vya ukatili katika jamii kwenye nyumba salama ya Wote Sawa iliyoko Wilayani humo.
Naibu Waziri Mwanaidi amesema kuwa jamii inatakiwa kutoa taarifa dhidi ya vitendo vyote vya ukatili wa kijinsia hususan kwa wanawake na watoto ili kuwawezesha wahanga wa vitendo hivyo kupata haki yao.
“Serikali inaandaa mazingira ya kukabiliana na vitendo ya ukatili dhidi ya wanawake na watoto, kwa hiyo msikae kimya dhidi ya ukatili wa vitendo hivyo, Tumieni mifumo iliyopo kutoa taarifa na Sheria iweze kuchukua mkondo wake na wahanga hao kupata haki”alisema Niabu Waziri Mwanaidi.
Vilevile amesema kuwa ukimya katika jamii dhidi ya vitendo hivyo una madhara makubwa kwa waathirika na wakati mwingine ukimya huo unasababisha kutoweka kwa ndoto za waathirika katika maisha yao baadaye kutokana na kuathirika kimwili na kisaiklojia.
Amependekeza mifumo iliyopo katika kusimamia na kuchunguza mashauri ya unyanyasaji wa kijinsia kuangaliwa upya kwa kuwa muda uliowekwa ni mwingi ilhali wahanga wanakuwa wakiteseka kwa muda mrefu kabla ya mashauri hayo kufanyiwa kazi kikamilifu na kufikishwa mahakamani.
Akizungumza kuhusu uendeshaji wa nyumba salama ya Wote Sawa, Meneja wa nyumba hiyo Jaqueline Ngalu amesema hatua iliyofikiwa ni kutokana na Serikali kwa kushirikiana na wadau kuandaa mwongozo wa kitaifa kuanzisha na kuendesha nyumba Salama.

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.