MTANGAZAJI

NCHI ZA KIAFRIKA KUPELEKA AGENDA YA MAENDELEO YA KIDIGITALI BENKI YA DUNIA NA IMF

 


 Mawaziri wa Fedha na Uchumi na Magavana wa Benki Kuu kutoka nchi 54 barani Afrika ikiwemo Tanzania, wamekutana mjini Bujumbura nchini Burundi katika Mkutano wa 58 wa Afrika ili kujadili namna ya kulishawishi Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF na Benki ya Dunia, pamoja na mambo mengine, kuziwezesha nchi za Afrika kujenga miundombuni ya kidijitali ili kukuza uchumi wa nchi hizo baada ya changamoto ya ugonjwa wa Uviko-19.

Ujumbe wa Tanzania katika Mkutano huo umefanyika katika Jengo la Bunge la nchi ya Burundi (Kigobe) na kufunguliwa na Rais wa Jamhuri ya Burundi, Generali Evariste Ndayishimiye, unaongozwa na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhandisi Hamad Yussuf Masauni kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania Profesa Frolens Luoga.

Lengo la mkutano huo ni kujadili namna ya kuzishawishi taasisi za fedha za kimataifa ikiwemo Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF na Benki ya Dunia kuziwezesha nchi za Afrika kukabiliana na kasi ya mabadiliko ya kiteknolojia hususan katika suala la biashara ya mtandao, uchumi wa kidigitali na ujenzi wa  miundombuni ya kidijitali ili kuweza kuifikia sehemu kubwa ya wanachi mijini na vijijini.

Mkutano huo ambao umebebwa na dhima isemayo “umuhimu wa mifumo ya kidigitali katika kukuza uchumi shirikishi na endelevu” (digitalization for inclusive recovery and sustainable growth) ni sehemu ya maandalizi ya Mkutano wa mwaka wa Benki ya Dunia na Shirika la Fedha Duniani IMF unaotarajiwa kufanyika mwezi Oktoba mwaka 2021.

Naibu Waziri wa Fedha na Mipango
Hamad Yussuf Masauni alisema kuwa wakati wa kilele cha Mkutano huo, Magavana hao wa IMF na Benki ya Dunia, wanatarajia kuweka msimamo wa pamoja juu ya vipaumbele vya Bara la Afrika na  namna taasisi hizo za kimataifa zinaweza kusaidia nchi hizo kupata rasilimali fedha za kuwekeza katika miundombinu ya kidigitali, mifumo na sera rafiki zitakazowezesha wananchi kuwa na uwezo wa kutumia teknolojia za kidijitali katika kufanya shughuli zao za kiuchumi na kijamii.

Alisema kuwa kizazi kilichoelimika kuhusu matumizi ya kidigitali, kinachangia maendeleo na kubuni nyenzo zinazosaidia kutekeleza kazi za ubunifu zitakazosaidia kukuza ajira na kuboresha maisha ya wananchi.

Alizungumzia pia suala la umuhimu wa kufua umeme kutokana na vyanzo vya gharama nafuu kama maji na gesi asilia pamoja na kuhakikisha kuwa huduma hiyo ya umeme inawafikia wananchi wengi ili uwezeshe upatikanaji wa huduma za kidigitali. Mheshimiwa Masauni pia alisema kuwa, kutokana na changamoto kadhaa ikiwemo ya umeme na miundombinu ya kidigitali, robo tatu ya wakazi bilioni 1.3 Barani Afrika hawatumii Intaneti jambo linalokwaza wananchi kutumia fursa za kidijitali katika kuendesha maisha yao hususan katika kipindi hiki cha changamoto ya ugonjwa wa Uviko-19.

Mhandisi Masauni alifafanua kuwa hivi karibuni Benki ya Dunia imekubali kuipatia Tanzania mkopo nafuu wenye thamani ya dola za Marekani milioni 150 kwa ajili ya kuboresha upatikanaji wa huduma za mtandao wa intaneti kupitia mkongo wa taifa kwa ajili ya matumizi ya Serikali, sekta ya biashara na wananchi na kwamba watatumia maazimio hayo kuiomba Benki ya Dunia iongeze kiwango cha fedha kwa ajili ya kutekeleza mradi huo pamoja na kuboresha miundombinu ya umeme ambayo ni muhimu katika kutekeleza miradi ya kidigitali kupitia madirisha ya IDA 19 na IDA 20.

“Tumelenga kwamba ifikapo mwaka 2025 tuwe tumefikisha mtandao wa intaneti kwa zaidi ya asilimia 80 kwa watanzania wote na kuhakikisha sekta hiyo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano inachangia pato la Taifa kwa asilimia 3 badala ya asilimia 1.5 za sasa” alifafanua Mhandisi Masauni.

Alisema kuwa Mambo yaliyojadiliwa kutokana na mawasilisho kutoka kwa wataalam mbalimbali yamegusa maeneo ambayo nchi za kiafrika zikiyafanyiakazi yatachangia Bara la Afrika kukuza uchumi wake na kuondokana na umasikini.

Mkutano huo wa 58 wa Magavana wa IMF na Benki ya Dunia unaofanyika Bujumbura Burundi ambapo kutokana na hali ya janga la UVIKO 19, baadhi ya nchi zilihudhuria na nyingine hazikuweza na hivyo kushiriki kwa njia ya mtandao, umehudhuriwa pia na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango anayeshghulikia masuala ya Fedha za Nje Bi. Amina Khamis Shaaban na Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-Fedha na Mipango- Zanzibar Bw. Aboud Hassan Mwinyi.

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.