MTANGAZAJI

MAJALIWA AWATAKA WATANZANIA KUSHIRIKI ZOEZI LA SENSA 2022

 

Waziri Mkuu wa Tanzania  Kassim Majaliwa ametoa wito kwa wananchi nchini humo kushiriki kikamilifu katika zoezi la Sensa ya Watu na Makazi linalotarajiwa kufanyika mwaka 2022 ili kuiwezesha Serikali kupanga maendeleo, kupunguza umasikini na kukuza uchumi.

Majaliwa ametoa rai hiyo jijini Dodoma wakati akizindua Kitabu cha Mkakati wa Usimamizi wa Utekelezaji wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022 kilichoandaliwa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS).
“Matokeo ya sensa yataiwezesha Serikali kupata takwimu za msingi zinazotumika kuakisi hali halisi iliyopo na kupanga mipango ya maendeleo kwa kutunga sera pamoja na kupanga mipango, program na kufuatilia utekelezaji wake”, alisema Mhe. Majaliwa.
Alisema ni muhimu wananchi watoe ushirikiano kwa wakusanya takwimu ili kuliwezesha zoezi hilo kuenda vizuri na kuleta matokeo tarajiwa kwa maendeleo ya nchi.
Amewataka Wakuu wa Mikoa na Wilaya nchini Tanzania kuanza kutoa elimu ya umuhimu wa sensa kwa wananchi ili kuwaweka tayari kushiriki zoezi hilo muhimu kwa maendeleo ya nchi hiyo.
Kwa upande wake Makamu wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Hemed Suleiman Abdallah alisema kuwa kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, sensa ya watu na makazi ni miongoni mwa sehemu muhimu katika Muungano wa Tanzania.
Alisema anaamini kuwa sensa ya mwaka 2022 itakuwa ya kipekee kutokana na juhudi za viongozi na wataalamu waliopo ambao wamesha ainisha changamoto zote zilizojitokeza katika sensa zilizopita na kupanga namna bora ya kuzitatua kwa ajili ya kuboresha.
Naye Naibu Waziri wa Fedha na Mipango,Mhandisi Hamad Yussuf Masauni  alisema Serikali inawajibu wa kuandaa zoezi la sensa ya watu na makazi ili kupata idadi kamili ya watu na kuweza kupanga maendeleo ili kukuza uchumi.
Alimhakikishia Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa kuwa Ofisi za Taifa za Takwimu za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Zanzibar zitahakikisha zoezi hilo linafanyika kwa ufanisi mkubwa.
Awali Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Emmanuel Tutuba alisema kuwa Uzinduzi wa Kitabu cha Mkakati wa Usimamizi wa Utekelezaji wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022 ni alama kuu ya uzinduzi rasmi wa shughuli za maandalizi ya sensa hiyo ambayo majaribio yake yatafanyika Agosti, 2021.
Mtakwimu Mkuu wa Serikali, Dkt. Alibina Chuwa alisema sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 ni sensa ya sita kufanyika nchini ambapo sensa ya kwanza ilifanyika 1967, ya pili 1978, ya tatu 1988, ya nne 2002 na ya tano 2012.
Alisema Sensa hiyo itakuwa ya kipekee kwa kuwa itatumia teknolojia ya hali ya juu ili kupata taarifa kuanzia kwenye ngazi ya vitongoji, vijiji na ngazi ya mitaa na mijini wakikusanya taarifa sahihi za idadi ya watu, umri, elimu na upatikanaji wa huduma za kijamii kama maji, umeme na afya.

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.