MTANGAZAJI

COSOTA YATOA ANGALIZO KWA VITUO VYA TELEVISHENI TANZANIA



 Uongozi wa Taasisi ya Hakimiliki Tanzania (COSOTA) umetoa angalizo kwa vituo vya Televisheni nchini humo vinavyonunua Tamthilia na Filamu kuhakikisha wanahakiki Umiliki wa kazi hizo COSOTA kabla ya kuzirusha.


Wito huo umetolewa Jijini Dar es Salaam hivi karibuni na Mwanasheria wa
COSOTA  Bw.Lupakisyo Mwambinga katika kikao cha kutatua mgogoro  kati ya
Muandaaji wa Tamthilia Likuru the Village Elders iliyoandaliwa na  Kampuni ya
Ladha ya Mtaa ya nchini Kenya, ambapo tamthilia hiyo ilirushwa na televisheni ya Clouds Plus TV  hivi sasa Plus TV ya nchini Tanzania ilirusha  kazi hiyo bila ya
kuhakiki Umiliki baada ya kuinunua kazi hiyo kutoka wakala aliyewauzia na kujikuta wameingia katika mgogoro huo.

"COSOTA imekuwa ikitoa huduma ya kuhakiki umiliki wa kazi zote za Sanaa na
Ubunifu ikiwemo kwenye Filamu na Muziki hivyo ni vyema kila unaponunua Filamu yoyote au tamthilia ilete COSOTA tukusaidie kukagua umiliki wake kwa lengo la kuepuka migogoro na kulipa faini kubwa kutoka kwa mmiliki halali wa kazi hiyo"alisema Mwambinga.

 Mwendeshaji wa Vipindi kutoka kituo cha Plus Tv zamani Clouds Plus Tv Bw.Isaya Kandonga  ametoa angalizo kwa Wafanyabiashara kuwa makini wanaponunua kazi hizo kutoka kwa mawakala mbalimbali. 

"Pongezi kwa uongozi wa COSOTA  kwa namna walivyosimamia mgogoro huu  na kuhakikisha tunamaliza kesi hii kwa maridhiano mazuri na kupitia kesi hii uongozi wa Plus Tv umejifunza kwa sasa kwa kila Filamu au Tamthilia tunayonunua tutahakikisha tunaiwasilisha COSOTA kwa ajili ya kuhakiki umiliki wake" Bw.Kandonga.


Katika kikao hicho Bw.Kandonga alieleza kuwa uongozi umeridhia kulipa kiasi cha Shilingi Milioni Sita, pamoja na gharama nyingine  kwa mmiliki wa kazi hiyo Bw. Ayuko ikiwa ni fidia ya kurusha kazi hiyo bila ya kuingia makubaliano na mmiliki huyo.

 Muandaaji wa Tamthilia hiyo ya  Likuru the Village Elders kutoka Kenya alipongeza na kushukuru uongozi wa COSOTA kwa namna walivyomsadia kupata haki yake.


Halikadhalika kufuatia mashirikiano mazuri ya Taasisi ya COSOTA na nchini
nyingine,  mlalamikaji aliwasiliana na ofisi ya Hakimiliki Kenya (Kenya Copyright Board - KECOBO) na kupewa barua ya utambulisho kuja COSOTA na alipofika katika ofisi hizo Tanzania alisaidiwa vyema malalamiko yake.

Hivyo basi COSOTA inatoa rai kwa Wasanii wote watanzania kutosita kufika katika ofisi zao kuomba msaada wa kisheria pale wanapopata changamoto yoyote ya kazi zao kutumika popote ndani na nje ya nchi bila ya kuwepo na makubaliano.

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.