MTANGAZAJI

WAZIRI AIPA MIEZI MITATU MAMLAKA YA MAWASILIANO TANZANIA KUTATUA MALALAMIKO YA WANANCHI

Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dkt. Faustine Ndugulile akisisitiza jambo
kwa Menejimenti ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (hawapo pichani), wakati
alipotembelea taasisi hiyo, Dar es Salaam

Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dkt. Faustine Ndugulile (wa pili kushoto) na
Naibu Waziri wake, Mhandisi Kundo A. Mathew (wa tatu kushoto) wakimsikiliza Mhandisi
Jumanne Ikuja akiwaeleza kuhusu gari lenye mitambo maalumu linalofuatilia matumizi ya
masafa wakati wa ziara yao Mamlaka ya mawasiliano Tanzania, Dar es Salaam. Wa nne
kushoto ni Mkurugenzi Mkuu wa taasisi hiyo, Mhandisi James Kilaba

 Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari nchini Tanzania, Dkt.Faustine Ndugulile ameipa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) miezi mitatu kumaliza tatizo la bando na vifurushi vinavyotolewa na kampuni za simu za mkononi nchini humo kwa wananchi.


Dkt. Ndugulile ameyasema hayo wakati wa ziara yake alipotembelea TCRA ikiwa ni moja ya taasisi zilizo chini ya Wizara hiyo kwa lengo la kufahamiana, kutambua majukumu yao na kuzungumza na Bodi, Menejimenti na wafanyakazi wa taasisi hiyo ili kuwa na uelewa wa pamoja na kushirikiana kwa kufanya kazi kwa pamoja katika kuhudumia wananchi kuelekea Mapinduzi ya Nne ya Viwanda na kuiwezesha Tanzania kuwa na uchumi wa kidijitali.


Ameongeza kuwa TCRA ishughulikie malalamiko ya wananchi kwa kuwa wananchi hawana imani na vifurushi na bando, na kuwe na mfumo wa kuhakiki gharama halisi za mawasiliano kuendana na fedha aliyotoa mwananchi na kuwe na namba ya bure ambayo wananchi watapiga ili kuwasilisha malalamiko yao ili kuwawezesha wananchi kuongeza imani yao kwa Serikali.


Amesisitiza kuwa ni heri tufanye maamuzi mabaya kuliko kutokufanya maamuzi na amewataka washirikiane na Baraza la Watumiaji wa Huduma za Mawasiliano (TCRA – CCC) kumaliza changamoto hiyo kwa kuwa watanzania sio wajinga, anataka aone kapata shilingi moja anaitumia shilingi moja yake kupiga simu.


Pia, amehimiza wahakikishe kuwa chaneli tano za bure za runinga zinaonekana Tanzania hata baada ya muda wa kulipia kumalizika kwa kuwa chaneli hizo hazionekani kwenye baadhi yaving’amuzi.


 Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Mhandisi Kundo A. Mathew ameipongeza TCRA kwa kutengeneza mifumo ya TEHAMA, kutambua changamoto zilizopo na imejipanga kuzifanyia kazi kwa kuwa lazima TEHAMA ichukue nafasi yake na itufikishe watanzania tunakotaka kwenda.


Naye Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt.Zainab Chaula amewataka wafanyakazi wa TCRA kujiongeza na kujituma zaidi badala ya kusubiri maagizo na maelekezo kwa   kuwa wao ni wataalamu, hivyo washirikiane kwa pamoja ili kuhakikisha kuwa wanaendelea kuwahudumia watoa huduma na watumiaji wa huduma za mawasiliano.


Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Mhandisi James Kilaba amekiri uwepo wa changamoto za bando na vifurushi na ameahidi kuzifanyia kazi kwa kuwa TEHAMA imeongeza mnyororo wa thamani kwenye sekta zote na imesogeza huduma mbali mbali viganjani.

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.