MTANGAZAJI

NAIBU SPIKA WA BUNGE LA TANZANIA AKEMEA VIPIGO KWA WANAWAKE

 

Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Tulia Ackson (kushoto) akiangalia muonekano wa GBV APP iliyotengenezwa kwa ajili ya kupata taarifa za Ukatili wa Kijinsia wakati wa Uzinduzi wa Siku 16 za kupinga Ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto jijini Dar es Salaam kulia mwenye koti ni Katibu Mkuu Wizara ya Afya - Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii Dkt. John Jingu.

Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Tulia Ackson amekemea vitendo vya kupigwa kwa Wanawake na Watoto wa kike vinavyotokea katika Jamii.

 

Dkt. Tulia ameyasema hayo leo jijini Dar es Salaam wakati akizindua Kampeni ya Siku 16 za kupinga Ukatili yenye Kauli mbiu isemayo: Tupinge vitendo vya Ukatili: Mabadiliko yananza na mimi.

 

Dkt. Tulia amesema kuwa Jamii inatakiwa kuanza kutambua mchango wao katika juhudi za Serikali katika mapambano dhidi ya vitendo vya Ukatili vinavyotokea katika jamii.

 

"Jamii tuchukue hatua zaidi haya yanayotokea katika Jamii tunaweza tukayaponga na kuyakataa ndio maana tunasema mabadiliko yananza na mimi" alisema.

 

Amesema Serikali ya Tanzania imekusudia kuendelea kushirikiana na Mashirika ya Kimataifa na Kitaifa ili kuhakikisha vitendo vya Ukatili katika jamii vinatokomezwa nankutoweka katika Jamii.

 

Dkt. Tulia ameitaka jamii kuwapa fursa watoto wa kike sawa na watoto wa kiume katika nyanja mbalimbali hasa katika kupata elimu na kusisitiza Jamii kuwaheshimu Wanawake na Watoto wa kike.

 

Akizungumzia utekekezaji wa Mipango mbalimbali ya Kutokomeza Vitendo vya Ukatili Katibu Mkuu Wizara ya Afya- Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii Dkt. John Jingu amesema Serikali itaendelea kushirikiana na Wadau katika kuhakikisha vitendo vya ukatiki dhidi ya wanawake na Watoto vinatokomezwa nchini.

 

"Tutaendelea kutilia mkazo suala hili kwa nguvu zaidi na kutafuta namna mbalimbali za Mapambano ya Kutokomeza Vitendo vya Ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto" alisema

 

Naye Mkurugenzi wa Wildaf Anna Kulaya amesema kuwa Wanawake wa vijijini na hasa wenye elimu duni wamekuwa wakifanyiwa vitendo vya kikatili hivyo jitihada kubwa zinahitajika katika kuhakikisha Jamii hiyo unapata elimu ya kutokomeza vitendo vya kikatili.

 

"Utashangaa sana hata katika Vyuo na Vyuo vikuu kumekuwa na taarifa nyingi za uwepo wa vitendo vya kikatili kwa wanafunzi katika Vyuo hasa uwepo wa rushwa ya ngono" alisisitiza

 

Wakati huo huo Mhe. Tulia Ackson alizindua GBV APP maalum kwa ajili ya wananchi kutoa na kupata taarifa mbalimbali kuhusu vitendo vya ukatili ikiwemo elimu juu ya mapambano dhidi ya vitendo hivyo.

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.