MTANGAZAJI

DAR ES SALAAM:SERIKALI YATOA UFAFANUZI KUHUSU SAFARI ZA RAIS JAKAYA KIKWETE NJE YA NCHI

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Safari za Mhe. Rais Jakaya Mrisho Kikwete Nje ya Nchi

Wizara imesikitishwa na taarifa za uongo zilitolewa katika vyombo vya habari kuwa Mhe. Jakaya Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika uongozi wake wa miaka 10 ametumia Shilingi trilioni 4 kwa ajili ya safari za kikazi nje ya nchi, ambazo ni wastani wa bajeti nzima ya wizara kwa miaka mitano (5).

Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa inapenda kutoa ufafanuzi kuwa tangu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete aingie madarakani mwaka 2005, kiasi kikubwa kabisa cha bajeti kuwahi kutengwa kwa ajili ya safari za Viongozi Wakuu yaani Rais, Makamu wa Rais na Waziri Mkuu ni shilingi bilioni 50 ambazo zilitengwa kwa Mwaka wa Fedha 2014/2015 kwa ajili ya Idara ya Itifaki. Kwa miaka mingine yote wastani umekuwa ni kati ya shilingi bilioni tano hadi 25 kulingana na mahitaji ya idara hiyo.


Ifahamike kuwa kiasi hicho cha shilingi bilioni 50 ni bajeti nzima ya Idara ya Itifaki, ambapo kuna fungu maalum kwa ajili ya ziara za viongozi. Fungu hilo linagharamia makundi makuu matano kama ifuatavyo:
    •    Kundi la Rais wakiwemo Wasaidizi, Mawaziri au Wakuu wa Taasisi na Walinzi;
    •    Kundi la Makamu wa Rais wakiwemo Wasaidizi, Mawaziri au Wakuu wa Taasisi na Walinzi;
    •    Kundi la Waziri Mkuu wakiwemo Wasaidizi, Mawaziri au Wakuu wa Taasisi na Walinzi;
    •    Kundi la Wakuu wa Nchi na Serikali kutoka nje ya nchi wanapotembelea Tanzania; na
    •    Kundi la Wajumbe Maalum wanaokuja nchini kuleta taarifa muhimu kwa Rais.
Makundi yote haya hugaramiwa na Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Nje ndani ya bajeti ya Idara ya Itifaki kifungu cha Ziara za Viongozi. 

Aidha uandaaji wa bajeti ya Wizara chini ya Idara ya Sera na Mipango unahusisha wadau wengine nje ya Wizara kama vile Kamati ya Bunge ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na hupitishwa kila mwaka na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Tunapenda kuwaatahadharisha wananchi juu ya watu wanaotoa taarifa za uongo kwa madhumuni ya  kujenga chuki dhidi ya Serikali.  Ikumbukwe kuwa ziara za viongozi zinazoratibiwa na Wizara ya Mambo ya Nje zina mafanikio makubwa kwa nchi na Watanzania kwa ujumla.

Wizara inaandaa taarifa ya ndefu ya utekelezaji wa majukumu ya Wizara, changamoto na mafanikio yaliyopatikana ndani ya kipindi cha miaka kumi ya uongozi wa Rais Jakaya Mrisho Kikwete ambayo itatolewa kwa umma kwa lengo la kutoa elimu zaidi. 

MWISHO.
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali kwa Umma,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa,
17 Septemba 2015

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.