MTANGAZAJI

DAR ES SALAAM:WAWILI WAKAMATWA KWA TUHUMA ZA UJAMBAZI



Watu wawili wamekamtwa kwa tuhuma za mauaji ya Sista Clesencia Kapuli (50) wa Kanisa Katoliki,  aliyekuwa Mhasibu katika Shule ya Sekondari Mwenyeheri, jijini Dar es Salaam.

Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, limesema watu hao ni kati ya watu wanane waliokamatwa kwa tuhuma za ujambazi sugu wa kutumia silaha.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Kamishna Suleiman Kova, amesema watu hao walikamatwa juzi  katika operesheni iliyofanywa na jeshi hilo kwa kutumia vikosi maalum.

Amesema licha ya watu hao wawili kuhusika katika tukio la mauaji ya sista huyo, lakini pia walihusika katika tukio la kupora fedha katika benki ya Barclays tawi la Kinondoni miezi michache iliyopita.

Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni ni Manase Ogenyeka (35), mkazi wa Tabata na Hamis Ismail, mfanyabiashara na mkazi wa Magomeni Mwembechai.

Pia Jeshi la Polisi limesema linaendelea na operesheni hiyo pamoja na kuwatafuta watuhumiwa wengine waliohusika katika tukio la maujai ya  sista Kapuli, Juni 23, mwaka huu, pamoja na mmoja aliyehusika katika tukio la wizi wa fedha katika benki ya Barclays.

Sista huyo ambaye  alikuwa mhasibu wa Shule ya Sekondari Mwenyeheri iliyopo Makoka wilayani Kinondoni, aliuawa Juni 23, mwaka huu  kwa kupigwa risasi na watu wanaosadikiwa kuwa ni majambazi waliokuwa katika pikipiki aina ya Boxer.


No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.