MTANGAZAJI

WANANCHI WA LUCHELELE MWANZA WATAKA MKUU WA KITUO CHA POLISI AONDOLEWE

Wakazi wa Luchelele,kata ya Mkolani,wilayani Nyamagana,wamemtaka Kamanda wa Polisi Mkoani Mwanza Valentino Mlowola kumchukulia hatua kali za kinidhamu Mkuu wa kituo cha Polisi cha Igogo,kufuatia kuachiwa huru watuhumiwa wa ujambazi,mauaji na ubakaji katika eneo hilo.
 
Wakizungumza jana katika Mkutano wa wananchi hao na Kamanda wa Polisi Mwanza,uliofanyika katika Shule ya Msingi Luchelele, wananchi hao wamesema hawana imani na Mkuu huyo wa kituo cha polisi cha Igogo,kufuatia matukio mengi ya uhalifu kutokea kila mara eneo hilo,bila watuhumiwa kuchukuliwa hatua za kisheria.
 
Wamemtaka Mkuu huyo wa Polisi Mkoani Mwanza kuwakamata upya watuhumiwa wa matukio ya ujambazi,ubakaji na mauaji yaliyotokea Feburuari 7 mwaka huu eneo hilo,lakini watuhumiwa wawili kati ya wanne wakaachiwa huru.
 
Ili kurejesha imani kati ya wananchi hao na jeshi la polisi,wananchi hao walitaka jeshi la polisi kufuatilia upya jalada la kesi hiyo.
 
Kamanda wa Polisi Mkoani Mwanza,Valentino Mlowola,mapema  wiki hii aliwaambia waandishi wa habari  kwamba watuhumiwa wawili kati ya wanne wa kesi hiyo waliachwa huru na ofisi ya Wakili wa Serikali Mkuu Mfawidhi Mkoani Mwanza,kulingana na taratibu na mfumo wa mwenendo wa makosa ya jinai.
 
Kamanda Mlowola amekubali kufanyia kazi madai ya wakazi wa eneo hilo,ikiwemo kumhamisha Mkuu huyo wa kituo cha Igogo,na kuwajengea kituo kipya cha polisi katika eneo la Luchelele,ili kudhibiti matukio ya uhalifu yanayotokea mara kwa mara eneo hilo.
 
Na:Conges Mramba-Mwanza

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.