MTANGAZAJI

SHIDA YA MAJI YAKIKUMBA CHUO CHA UALIMU TARIME,MARA





  Familia za wafanyakazi wa chuo cha ualimu Tarime wakisubiri kuchota maji ambayo sasa ni shida katika mji huo..
Chuo cha Ualimu Tarime kilichoko Wilayani Tarime mkoani Mara kiko hatarini kukumbwa na magonjwa ya mlipuko kutokana na uhaba wa maji  uliopo katika chuo hicho unaosababishwa na idadi kubwa ya wanachuo  zaidi ya 800 walioko chuoni hapo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na blog hii Wilayani humo, walisema kuwa wanahofia hali ya afya zao kutokana na wingi wa wanachuo ambao hutumia bomba moja linalofanya kazi kwa nguvu ya mashine ya kusukuma maji ambayo nayo kwa sasa haifanyi kazi kwa kuharibika.

“Tuna shida ya maji kutokana na mashine inayosukuma maji kuharibika na sasa tunaloa maji kwa kutumia ndoo kwa kupiga msitari na mara nyingi maji huisha bila sisi kuenea na kuamua kuingia darasani bila kuoga” alisema mmoja wa wanachuo hao bila kutaka kujwa jina lake.

Kutokana na ratiba ya chuo hicho kuwa finyu, wanachuo hulazimika kupewa muda mufupi wa kuchota maji na kuoga ambapo hawaenei kutokana na idadi kubwa iliyopo kwa sasa kwa kuwa chuo hicho kina uwezo wa kuchukuwa wanachuo 500 tu.

“Bweni la Kenyata lenye uwezo wa kubeba wanachuo 105 kwa sasa linawachuo wapatao 180 huku lile la Nkurumah lenye uwezo wa kubeba wanachuo 135 kwa sasa lina  jumla ya wanachuo 200 kutokana na uhaba wa mabweni” alisema mwanachuo huyo.

Aliongeza “tunalazimika  kulala wawili wawili katika kitanda kimoja jambo ambalo linaweza kuhatarisha afya zetu ukizingatia kuwa tumetoka katika familia tofauti tofauti na hatujuani afya zetu” aliongeza.

Historia inaonyesha kuwa Chuo cha ualimu Tarime kilianzishwa mwaka 1974 kama  chuo cha ualimu daraja la III C, mwaka 1981 serikali ilibadilisha programu na kuwa daraja la III B  ili kupata walimu wengi ambao waliitwa wa UPE (Universal Primary Education) huku wengine wakiuita ualimu huo kuwa ni Ualimu Pasipo na Elimu.

Aidha mwaka 1990 ulianzishwa rasmi mfumo wa Ualimu daraja la III A  ambao unaendelea mpaka sasa kwa miundo mbinu ile ile ya chuo iliendelea kutumiwa bila kufanyiwa ukarabati hadi hivi sasa.

Hata hivyo wanachuo hao walisema kuwa japo chuo hicho ni kati ya vyuo vikongwe vya ualimu hapa nchini kulingana na historia yake,  bado miundo mbinu yake ni mibovu na inahitaji kufanyiwa ukarafati mkubwa ili kuendana na hadhi ya jina lenyewe.

“Huwezi amaini kuwa chuo hiki ambacho kinatoa wataalamu na watu maarufu katika nchi hii ndio kinamwonekano huu ambao hata wewe ukiingia ndani ya mabweni tunayolala utatuhurumia na tunatoa fedha za ukarabati kwa kila mwaka shilingi 10,000/= kwa kila mwanchuo ukipiga hesabu hizo fedha ni kiasi gani?”alihoji mwanachuo mwingine wa mwaka wa pili.

Wanachuo hao walieleza kuwa kero  hiyo ni la miaka na mikaka ingawa kila wanapohoji huambiwa wao ni chadema na kwa kuwa wameenda kutafuta mafunzo yenye ajira huamua kunyamaza huku roho zikiendelea kuwauma kwa kukosa pa kusemea.

“Tunazibwa midomo hatuwezi kuongea kwa madai kuwa anayeongea ni CHADEMA wakati hali halisi inayotukabili inaonekana wazi. Na kutokana na hili  inaonesha wazi kuwa chuo nacho kimeingia kwenye siasa bila sisi kujuwa” alisema mwanachuo huyo wakati wa mahojiano akiwa kwenye zoezi la utafiti wao wa kielimu kama sehemu ya kukamilisha kazi yao ya mafunzo ya ualimu daraja la III A.

Mabweni ya wanachuo wa kiume hayana madirisha hali inayokuwa tete zaidi ni wakati mvua inapoanza kunyesha hasa yenye upepo maji hujaa ndani huku Godoro na shuka za wanachuo kulowana.

“Tunaomba serikali iangalie chuo hiki ikipangie bajeti ya kukifanyia ukarabati ili wanachuo tufurahie kusomea ualimu lakini sasa ukiingia bwenini tumeziba madirisha kwa maboksi !” Mmoja  wa wanachuo hao aliongea akionyesha  masikitiko.

Mkuu wa chuo hicho Bw. Nicolaus Magige alipotakiwa kuyazungumzia matitizo yanayokikabili chuo chake  alikana kuwepo kwa matatizo  huku akikiri kuwepo kwa miundo mbinu mibovu ya maji.

“Hatuna shida na siwezi kuilaumu idara maji ya Wilaya ya Tarime kuwa chuo changu kinaupungufu wa maji ila miundo mbinu ya maji ni ya zamani inahitaji ukarabati ili kufanya  kazi  vizuri” alisema Bw. Magige kwa njia ya simu.
 Na Waitara Meng'anyi-Tarime

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.