MTANGAZAJI

SHERIA ZINAZOWAHUSU WAMACHINGA KUTAFSIRIWA KWA KISWAHILI

 


Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum kwa kushirikiana na Shirikisho la Umoja wa Wamachinga (SHIUMA), imeazimia kuhakikisha sheria ndogo zinazowahusu wamachinga zinatafsiriwa kwa lugha ya Kiswahili ili Wamachinga wote waweze kuzielewa.

Maazimio hayo yamefikiwa wakati wa kuhitimisha kikao cha siku mbili kati ya Wizara na Viongozi wa SHIUMA kutoka Mikoa ya Tanzania Bara kilichoongozwa na Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. Zainab Chaula kilichofanyika Jijini Dodoma.

Akifunga kikao hicho, Dkt. Chaula amewataka Wamachinga kushirikiana na Serikali kutekeleza maazimio waliyojiwekea kwa wakati kwa maslahi yao na Taifa kwa ujumla.

" Kufikia Machi  16  wanasheria wa SHIUMA kwa kushirikiana na wanasheria wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum na Ofisi ya Rais TAMISEMI wakamilishe kutafsiri Sheria hizo" amesema Dkt. Chaula.

Dkt. Chaula ameyataja maazimo ya kikao hicho kuwa ni pamoja na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum iboreshe madawati ya kushughulikia masuala ya Wamachinga kwa kushirikiana na Ofisi Rais TAMISEMI hadi Halmashauri, ili kusaidia kutatua changamoto kwenye maeneo yao.

Ameyataja maazimio mengine kuwa ni Wizara kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais TAMISEMI kuhakikisha Mamlaka za Serikali za Mitaa zinapanga na kuweka miundombinu wezeshi katika maeneo ya shughuli za Wamachinga kwa kushirikiana na Viongozi wa Wamachinga wa eneo husika, kuandaa kanzidata ya Wamachinga na Wizara kutembelea maeneo ya masoko ya Wamachinga ili kutatua changamoto zilizopo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa SHIUMA Taifa, Ernest Matondo ameishukuru Serikali kwa kuwakutanisha Wamachinga na kuahidi kushirikiana na Viongozi pamoja na Wamachinga mikoa yote ili kufanikisha kufika mbali na kutoka katika umachinga na kuwa wafanyabishara wa kati na wakubwa.

Naye Mkurugenzi wa Idara ya Serikali za Mitaa kutoka Ofisi ya Rais TAMISEMI Nuru Namoroma amewahakikishia Wamachinga wote kuwa Ofisi hiyo itaendelea kuratibu masuala yao kwa ufanisi zaidi katika ngazi ya Serikali za Mitaa kwa kushirikiana na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum ili wawe na mazingira mazuri ya kufanya biashara.

Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum kwa kushirikiana na SHIUMA kuratibu maadhimisho ya wiki ya Wamachinga itakayofanyika tarehe 29 Juni kila mwaka.


No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.