MTANGAZAJI

MAKAZI YA WAZEE TANGA KUKARABATIWA



Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum imeazimia kukarabati makazi ya wazee ya Muheza mkoani 
 Tanga hivi karibuni ili kuimarisha mazingira ya kuishi kwa wazee wanaolelewa katika makazi hayo.

Akizungumza na wazee hao alipotembelea makazi hayo Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. Zainab Chaula amesema wazee wana haki ya kupata huduma bora kwa ustawi wa afya zao.

Dkt. Chaula amewahakikishia wazee hao 20 wanaoishi kwenye makazi hayo kuwa muda si mrefu shughuli ya kukarabati majengo na miundombinu ya umeme, maji na barabara itaanza.

Ameongeza kuwa, Serikali haijawaacha wazee kwa kuhakikisha wanaishi vizuri katika makazi yote 14 yaliyopo nchini hivyo ziara yake ina lengo la kuona namna ya kuboresha makazi hayo ili yafanane na ustawi wa nchi.

"Tumekuja kuangalia ni namna gani  tutaboresha makazi haya yafanane na nyumba nzuri tunazopenda kuishi, kwa hiyo Serikali imetupa jukumu la kuhakikisha ustawi wenu unaimarika" amesema Dkt. Chaula.

Awali, Afisa mfawidhi wa makazi hayo Mwamvita Kilima amebainisha kuwa, changamoto za makazi hayo ni maji, umeme, uzio na uchakavu wa majengo.

Hata hivyo Mwamvita amesema, anapata ushirikiano mzuri wa Halmashauri katika kuwatunza wazee hao hususani huduma za afya.

"Namshukuru Mkurugenzi wa Halmshauri na timu yake, wakati wa mlipuko wa ugonjwa wa Uviko wazee wote walipatiwa elimu na wote wamechanja ameongeza Mwamvita.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Muheza Issa Misumari aliyekuwepo kwenye Ziara hiyo, aliwahakikishia wazee hao kuwa,  Halmashauri itaendelea kuwaangalia na kutoa ushirikiano kwa kuwawekea mazingira bora zaidi.

Akizungumza kwa niaba ya wazee wenzake Mzee Joseph Misigaro ameishukuru Serikali hususani Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuwajali wazee.


No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.