DKT. CHAULA AWATAKA WAMACHINGA KUTUMIA TEKNOLOJIA
Katibu
Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum nchini Tanzania Dkt. Zainab Chaula amewataka Wamachinga kutumia fursa zilizopo nchini humo
ikiwemo Teknolojia ya Habari na Mawasiliano katika Shughuli zao ili
kupiga hatua kiuchumi.
Akifungua
kikao cha kuwajengea uwezo Viongozi wa shirikisho la Wamachinga,
kilichofanyika Jijini Dodoma Februari 22, 2022 Dkt. Chaula
amesema kwa sasa Teknolojia inakuwa kwa kasi hivyo uwezekano wa kupata
masoko na bidhaa umerahisishwa ikilinganishwa na kipindi cha Nyuma
ambapo Teknolojia ilikuwa duni.
Dkt.
Chaula amesema, fursa nyingine zilizopo ni pamoja na amani na utulivu
uliopo nchini, mikopo ya Maendeleo kutokana na mapato ya Halmashauri,
pamoja na ardhi.
Amewataka pia, kuimarisha ushirikiano miongoni mwao, Serikali na
Wadau wengine ili kukuza zaidi mitandao ya biashara zao na kuboresha
maisha kwani wao wenyewe ni fursa katika kukuza uchumi wa Taifa. Pia
wasikubali kutumiwa kwa namna yoyote ili kuwatenganisha.
Dkt.
Chaula amebainisha kuwa Serikali nchini humo imetoa jumla ya
sh. bilioni 5 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya Wamachinga hivyo
Serikali itahakikisha fedha hizo zinatumika kwa ufanisi.
Awali
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na
Makundi Maalum Amon Mpanju akitoa maelezo kuhusu kikao hicho amesema
hadi tarehe 31 Januari usajili wa shirikisho la machinga ulikuwa
umekamilika.
Mpanju
amesema lengo la kikao hicho ni kuwasikiliza na kuwapa fursa ya kupata
elimu ya masuala mbalimbali ili kuongeza ufanisi katika shughuli zao.
"Nia
ya Serikali ni kuhakikisha kundi hili linapata Maendeleo kupitia
shughuli zao hivyo kikao hiki kinawajengea uelewa wa mambo muhimu
ikiwemo sheria, kanuni na taratibu za Serikali" amesema Mpanju.
Kwa
upande wake, Mwenyekiti wa Shirikisho la Machinga nchini (SHIUMA),
Ernest Matondo, wameishukuru Serikali kupitia benki ya NMB kwa
kuwakutanisha kwani wana imani matokeo ya kikao hicho ni kuboreshwa
zaidi kwa mazingira ya shughuli zao.
"Miundombinu
kwenye masoko haijakaa vizuri, hivyo kama alivyosema Katibu Mkuu fedha
hizo zitaboresha miundombinu ili Wamachinga waweze kufanya kazi vizuri
zaidi, tunamshukuru pia Mhe. Rais kwa kulitambua kundi hili na kuliweka
katika Wizara mahususi" amesema Matondo.
Post a Comment