MTANGAZAJI

AGIZO LA TOZO KWA WAMILIKI WA SIMU TANZANIA

 

Waziri  wa Fedha na Mipango nchini Tanzania Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba ametoa  muda wa siku 14 kuanzia Julai Mosi 1 hadi 15 Julai, 2021, kwa watoa huduma wote wa Mitandao ya Simu kurekebisha mifumo yao na kuanza kutoza rasmi makato ya kodi  ili Serikali ianze kukusanya fedha ambazo amesema zitatumika kwa malengo yaliyokusudiwa ya kuwakwamua wananchi kutoka katika adha mbalimbali.

Nchemba ametoa agizo hilo alipokutana na kufanya mazungumzo na Chama cha Watoa Huduma wa Simu Tanzania (TAMNOA), na kuwaeleza kuwa kodi ya miamala ya simu na bando za mitandao inayotakiwa kuanza kutozwa na mitandao ya simu inalenga kila Mtanzania kuchangia mapato ya Serikali kwa ajili ya maendeleo ya nchi.
 
 “Kampuni za simu msichukulie makato haya kama kodi nyingine mnazowatoza wateja wenu bali Serikali iliamua kuweka makato haya kwenye miamala ya kuweka muda wa maongezi na kufanya miamala kwa njia ya simu ili kuwafanya Watanzania na watumiaji wengine wa simu kuchangia maendeleo ya nchi”alisisitiza Dkt. Nchemba.
 
Kwa upande wao Chama cha Watoa huduma za mitandao ya simu, waliiomba Serikali kupitia Wizara ya Fedha na Mipango iwape muda wa kurekebisha mifumo yao itakayotumika kukusanya tozo hizo kwa kuwa zoezi hilo linahitaji muda wa kiufundi.
 
Akizungumza kwa niaba ya Chama hicho, Mkurugenzi wa Uhusiano wa Kampuni ya Simu ya Vodacom Bi. Roselynn Mworia, alisema kuwa chama chao kimeupokea mpango huo kwa mikono miwili na kuwataka wateja wao kuiunga mkono Serikali kwa kuendelea kutumia huduma za kupiga simu na kufanya miamala ya simu.
 
 Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hivi karibuni, lilipitisha tozo ya kuanzia shilingi 10 hadi shilingi 10,000 kutozwa katika kila muamala wa kutuma au kupokea pesa na kiwango cha shilingi 10 hadi 200 kwa siku kila mteja anapoongeza salio la muda wa maongezi kwenye simu ambapo kwa pamoja, Serikali inatarajia kukusanya wastani wa shilingi trilioni1.7 kwa mwaka.



No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.