MTANGAZAJI

WAZIRI WA AFYA USO KWA USO NA KAMATI YA BUNGE TANZANIA

 

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima akitoa maelezo mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu majukumu na Muundo wa Wizara hiyo katika kikao cha Kamati hiyo kilichofanyika Jijini Dodoma.




Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii nchini Tanzania, kwa mara ya kwanza imekutana na wataalam wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto na kupokea taarifa za Muundo na majukumu ya Idara na vitengo ndani ya Wizara hiyo.

Taarifa hiyo imewasilishwa hivi karibuni jijini Dodoma na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima katika kikao kilichohudhuriwa na wataalam kutoka pande mbili zinazounda Wizara; Idara Kuu ya Afya na Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii.

Akiwasilisha taarifa ya Wizara mbele ya Kamati hiyo, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Dorothy Gwajima amesema pamoja na changamoto kadhaa, Wizara imetekeleza majukumu yake kwa kiwango kikubwa kuhakikisha wananchi wanapata maendeleo na kuondokana na matatizo yanayoweza kuzuilika.

DKt. Gwajima amesema Wizara imepokea maelekezo na maoni ya Wajumbe wa Kamati hiyo na kuahidi kutimiza wajibu kuzifanyia kazi hoja mbalimbali zilizowasilishwa katika kikao hicho.

Akizungumzia Uratibu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGOs), Katibu Mkuu Wizara ya Afya-Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii, Dkt. John Jingu amesema Mashirika hayo yanafanya kazi kubwa ya kuisaidia Serikali kufikisha huduma kwa Wananchi.

Ameongeza kuwa Serikali imekuwa ikitoa mafunzo kwa Wasajili Wasaidizi wa NGOs ili Mashirika hayo yaweze kutoa huduma zake kwa misingi ya Uzalendo na kuhakikisha yanafanya kazi kwa mujibu wa Kanuni Sheria na taratibu za nchi.

Mwenyekiti wa Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, Stanslaus Nyongo walihoji masuala mbalimbali yanayolenga katika maendeleo na Ustawi wa Watanzania huku wakieleza kuridhishwa na kazi zinazofanyika huku waikielekeza Wizara kuhakikisha inabainisha changamoto katika utekelezaji wa majukumu na kuziwasilisha ndani ya Kamati ili zitafutiwe ufumbuzi.

Baadhi ya masuala yaliyosisitizwa Wajumbe wa Kamati ni pamoja na suala la upatikanaji wa huduma ya Bima ya Afya kwa Watanzania wote, uhamasishaji wa wananchi kupima Virusi vya Ukimwi kwa hiari, mwendelezo wa matumizi ya dawa za kufubaza virusi vya Ukimwi (ARV) pamoja na kubuniwa kwa mbinu za kukabiliana na tatizo la mimba katika umri mdogo.

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.