MTANGAZAJI

MAKAMPUNI YA SIMU TANZANIA YAONYWA KWA KUVUJISHA TAARIFA BINAFSI

 Telecommunication company in Tanzania

Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari nchini Tanzania Dkt. Faustine Ndugulile ametoa onyo kwa watoa huduma za mawasiliano nchini humo kuacha tabia ya kuvujisha taarifa binafsi za wateja kwa kuwadhibiti baadhi ya watumishi wao wasio waaminifu.


Ndugulile amebainisha hayo wakati akizungumza na watoa huduma za mawasiliano katika hafla ya kutia saini Mkataba baina yao na Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) wa kupeleka huduma za mawasiliano katika vijiji 173 vilivyo katika mikoa 16 nchini.


Amesema kuwa hapendezwi na tabia ya baadhi ya watumishi wa makampuni hayo
kuchapisha taarifa binafsi za wateja na kuzitoa kwa wagomvi wao na kwa watu wasio na nia njema.


“Niwaombe sana makampuni ya simu, someni vizuri sheria, vyombo vya dola ndivyo vinavyoruhusiwa kupata taarifa binafsi za mteja kwa malengo mahsusi na sio vinginevyo”, alisisitiza Ndugulile.


Ameongeza kuwa suala hilo atalisimamia kwa umuhimu wake na kampuni ya simu itakayotolewa malalamiko na wananchi kwa kuvujisha taarifa zao, hatua kali zitachukuliwa dhidi ya kampuni husika.


Kwa upande wa Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Mhandisi Andrea Kundo ametoa rai kwa watoa huduma za mawasiliano kuwa watafiti na wabunifu kwa kufanya uwekezaji kwa kutumia teknolojia nyepesi itakayowezesha mawasiliano ya uhakika kwa wananchi.

Mtendaji Mkuu wa UCSAF, Justina Mashiba amesema kuwa Serikali kupitia Mfuko huo imetoa ruzuku ya kiasi cha shilingi Bilioni 6 za kitanzania kwa makampuni ya simu ya Airtel, Vodacom na Tigo na kusaini Mkataba wa kupeleka mawasiliano katika vijiji 173 ifikapo Oktoba 2021.

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.