MTANGAZAJI

WHO:KIPINDUPINDU CHAWEZA KUDHIBITIWA


Wakimbizi wa Burundi wakipatiwa tiba dhidi ya Kipindupindu mkoani Kigoma nchini Tanzania. (Picha:© UNHCR/B.Loyseau)

Kipindupindu na tishio la mlipuko wake, imetajwa kuwa changamoto kwa afya ya umma katika nchi nyingi na kwa jamii ya kimataifa, wakati ugonjwa huo ukitajwa kuwepo katika nchi mbali mbali zikiwemo Tanzania, Sudan Kusini, Haiti, Nepal na Yemen kulingana na Shirika la afya duniani WHO katika taarifa yake ya mwezi julai mwaka huu.


Kulingana na Dkt. Dominique Legros, ambaye anasimamia  kitengo cha kipindupindu cha WHO, matumizi ya chanjo dhidi ya kipindupindu ni chombo muhimu katika kupambana na ugonjwa huo, kama ilivyodhihirika nchini Sudan Kusini.

Kulingana na takwimu za WHO zilizotangazwa na Radio ya Umoja wa mataifa mwezi julai mwaka huu ilieleza kuwa kuna visa vipya vinavyoshuhudiwa ambako nchini Haiti mwaka huu wa 2015 kufikia mwezi Juni visa 17, 812 ikiwemo vifo 150 vimeripotiwa. Nchini Tanzania, tangu kuzuka kwa mlipuko mwezi Mei mwaka huu, vimeripotiwa visa 4711, ikiwemo maambukizi ya waTanzania 182 yaliyochochewa na uhamiaji. Nchini Sudan Kusini kufikia mwezi Julai mwaka huu visa 632 vimeripotiwa ikiwemo vifo 30.


Leo hii vyombo vya habari nchini Tanzania vimeripoti kuwa serikali nchini humo imesema kuwa watu wawili wamekufa na wengine zaidi ya 30 wamelazwa katika hospitali za Mwananyamala na Sinza baada ya kuripotiwa  kulipuka kwa Ugonjwa wa kipindupindu katika Jiji la Dar es Salaam.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Mecky Sadiki kupitia Kituo cha Televisheni cha Taifa TBC1  amesema watu hao wawili waliofariki, mmoja ni mwanamume na mwingine ni mwanamke wanatokea Manispaa ya Kinondoni ambapo ugonjwa huo umethibitika baada ya vipimo vya maabara.

 Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni, Mussa Natty, amesema wagonjwa wengine 30 wapo chini ya uangalizi maalumu katika hospitali za Mwanayamala na Sinza, ambapo 19 wapo Sinza na 11 Hospitali ya Mwananyamala na Wengine wanne wameruhusiwa na kurudi nyumbani.

 Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa Dar es Salaam, Dk Jackson Makanjo, amewataka wakazi wa Dar es Salaam kuchukua tahadhari.


No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.