MTANGAZAJI

DAR ES SALAAM:AHUKUMIWA KIFUNGO CHA MIAKA 60 JELA KWA KOSA LA KUBAKA MTOTO



 court_gavel


Mahakama ya Wilaya ya Ilala jijini Dar es salaa imemhukumu Goodluck Aloyce (31) mkazi wa Tabata Msimbazi jijini humo , kifungo cha miaka 60 jela baada ya kupatikana na hatia ya kubaka na kumlawiti shemeji yake mwenye umri wa miaka 11 mara kwa mara.

Akisoma hukumu hiyo katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala, Hakimu Mkazi Mwandamizi, Juma Hassan amesema, mashahidi sita walioletwa na upande wa mashitaka waliisaidia mahakama kuthibitisha kwamba mshitakiwa alimbaka na kumlawiti mtoto huyo.

Amesema ripoti kutoka kwa daktari (PF3) iliyotolewa mahakamani hapo kama kielelezo, ilionesha kuwa mtoto huyo alikuwa akiingiliwa kimwili mara kwa mara na mshitakiwa.

Kabla ya kusomewa adhabu, Wakili wa Serikali, Felista Mosha aliitaka mahakama itoe adhabu kali kwa mshitakiwa ili liwe fundisho kwa wengine wanaofanya vitendo hivyo ambapo mshitakiwa aliiomba mahakama hiyo imwachie awe huru, ombi ambalo halikutiliwa maanani na mahakama hiyo.

Katika kesi hiyo, mshitakiwa alikuwa anakabiliwa na mashitaka mawili ya kubaka na kulawiti mtoto huyo mwenye umri wa miaka 11 kinyume na sheria.

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.