MTANGAZAJI

WAZIRI MKUU WA TANZANIA APONGEZA UBUNIFU WA MIFUMO YA FEDHA NA KUDHIBITI MAKOSA YA BARABARANI



Waziri Mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa alitembelea  banda la Serikali  katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) hivi karibuni na kujionea namna mifumo ya kielektroniki ya kukusanya maduhuli ya Serikali wa GePG unaosimamiwa na Wizara ya Fedha na mfumo wa Jeshi la Polisi wa kudhibiti wasiolipa faini za barabarani (TMS) inavyofanya kazi.


Waziri Mkuu aliwapongeza wabunifu wa mifumo hiyo ambayo kwa sasa inasaidia Serikali kupata mapato yake kwa wakati pamoja na kupunguza makosa ya barabarani ambayo yamekuwa yakiongeza ajali na kupunguza nguvu kazi ya Taifa.


Alisema uwekezaji katika Sekta ya Tehama ni muhimu  kwa nchi wanachama wa SADC ili kudhibiti uhalifu wa mtandaoni pamoja na kusimamia matumizi ya fedha za umma. 


Naye Mkuu wa Uendeshaji wa Mfumo wa GePG kutoka Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Basil Baligumya, alisema Wizara imeshiriki mkutano huo ili kuzionesha nchi mbalimbali zinazoshiriki mkutano huo namna Tanzania imepiga hatua katika maendeleo ya teknolojia hususani katika usimamizi wa fedha na ukusanyaji mapato ya Serikali kupitia mfumo wa GePG.


Bw. Basil alisema mfumo huo unadhibiti fedha za umma, umeongeza makusanyo na uwazi katika ukusanyaji wa mapato ya Serikali, pamoja na kuongeza usahihi wa taarifa za mapato.
 

Alisema kwa kuwa kubadilishana uzoefu ni miongoni mwa malengo ya mkutano huo, wako tayari kujifunza mbinu mpya za kuendeleza mifumo nchini pamoja na kuzielekeza nchi zitazokuwa tayari kujifunza namna ya kutengeneza mifumo ya kusimamia mapato ya nchi zao.


Kwa nyakati tofauti, washiriki mbalimbali waliotembelea banda hilo wameipongeza Serikali ya Tanzania  kwa kuanzisha mifumo hiyo ambayo itasaidia kudhibiti ubadhilifu wa fedha za umma, kukusanya mapato ya serikali kwa wakati pamoja na kudhibiti makosa ya barabarani.


Washiriki hao wamewapongeza watumishi wote walioshiriki katika kutengeneza mifumo hiyo kwani wameonesha uzalendo wa dhati kwa kuiwezesha Serikali kuweza kisimamia mapato yake kwa wakati.

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.