MTANGAZAJI

MBEYA:MCHUNGAJI RABSON NKOKO ACHAGULIWA MWENYEKITI MPYA WA SHC




 

Mkurugenzi wa mawasiliano wa kanisa la Waadventista Wa Sabato Unioni ya kusini mwa Tanzania Mchugaji Rabson Nkoko (Pichani) amechaguliwa hii leo kuwa mwenyekiti mpya  wa Konferensi ya Nyanda za juu Kusini mwa Tanzania  ya Kanisa hilo (SHC)

Uchaguzi huo unafuatia mabadiliko yaliyofanyika hivi karibuni ya kuundwa kwa konferensi mbili mpya baada ya kuvunjwa kwa iliyokuwa  konferensi ya mashariki mwa Tanzania ambapo aliyekuwa mwenyekiti wa konferensi hiyo Mchungaji Joseph Mngwabi alichaguliwa kuwa mwenyekiti mpya wa konferesi ya Mashariki na kati mwa Tanzania.

Mkurugenzi wa mawasiliano konferensi ya nyanda za juu kusini Mchungaji Haruni Kikiwa ameiambia Morning Star Radio kuwa zoezi  la uchaguzi huo lilianza kwa kuundwa kwa kamati ndogo ya uchaguzi ambayo ilikamilisha zoezi hilo majira ya saa sita mchana na kumtangaza mwenyekiti huyo.

Hii itakuwa ni mara ya kwanza kwa Mchungaji Nkoko kushika wadhifa huo,ambapo amewahi kuwa Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Unioni ya Tanzania na iliyokuwa Taasisi ya Vyombo vya Habari vya Kanisa la Waadventista Wa Sabato (TAMC) na Mchungaji wa Mtaa wa Kinondoni.

Akizungumza na Morning Star Radio mara baada ya uteuzi huo Mchungaji Nkoko amesema amepokea wadhifa huo kwa unyenyekevu na ameahidi kushirikiana na viongozi wengine katika kuwahimiza washiriki wa konferensi hiyo kumtafuta Mungu ambaye ndiye chanzo cha mafanikio.

Konferensi ya Nyanda za Juu Kusini mwa Tanzania ya Kanisa la Waadventista Wa Sabato (SHC) inawashiriki 46,000 na inajumuisha mikoa sita ya Tanzania bara.

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.