MTANGAZAJI

RELI YA KISASA TANZANIA NA BURUNDI

 


Serikali ya Tanzania na Burundi zimetia saini za awali za makubaliano ya pamoja ya utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) kutoka Uvinza Tanzania hadi Gitega Burundi yenye urefu wa kilomita 282.

Makubaliano hayo yamesainiwa mjini Kigoma na Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba na Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi,Prof. Makame Mbarawa kwa niaba ya Serikali ya Tanzania na Waziri wa Miundombinu, Ujenzi na Makazi, Dkt. Deogratius Nsanganiyumwami na Waziri wa Fedha, Bajeti na Mipango ya Uchumi, Mhe. Dkt. Domitien Ndihokubwayo, kwa niaba ya Serikali ya Burundi.

Akizungumza baada ya kutia Saini hizo, Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba alisema kuwa Serikali ya Tanzania na Burundi zimeanza kuangalia maeneo ambayo watapata fedha za kutekeleza mradi huo.

“Mimi na Waziri wa Fedha wa Burundi tunaanza kuangalia maeneo ambayo tunadhani tunaweza kupata fedha kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huu, tunawaambia watanzania, Warundi na maeneo mengine yatakayonufaika na reli hii kiuchumi kuwa fedha zitapatikana”, alieleza Dkt. Nchemba

Alisema Tanzania imekuwa na uzoefu wa kupata fedha za kutekeleza miradi mikubwa ya aina hiyo kama inayoendelea kwa kipande cha Dar es Salaam- Morogoro-Morogoro - Makutopora.

Dkt. Nchemba, alisema kuwa gharama za mradi huo zitatolewa baada ya kukamilika kwa taarifa za kihandisi lakini inakadiriwa kuwa hazitazidi dola za Marekani milioni 900.

Naye Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa, alisema kuwa reli hiyo itajengwa kwa kushirikiana na Burundi ambapo utekelezaji wake unatarajiwa kuanza hivi karibuni na inakadiriwa kuwa reli hiyo itakuwa inatumia treni za kisasa zenye mwendokasi wa kilometa 160 kwa saa.

Alisema kuwa upande wa Tanzania ujenzi wa reli utahusisha kuunganisha kipande cha Uvinza Malagarasi chenye urefu wa kilomita 156 ambapo Burundi wataanzia Malagarasi hadi Musongati – Gitega chenye urefu wa kilomita 126.

“Mradi huu ni muhimu kwa nchi yetu, Burundi na pia Congo ambao hutumia bandari ya Dar es Salaam kusafirisha mizigo, hivyo kukamilika kwa reli kutarahisisha usafirishaji wa mizigo kwenda katika nchi hizo,” alisema Prof. Mbarawa.

Kwa upande wa Burundi, Waziri wa Miundombinu, Ujenzi na Makazi, Dkt. Deogratius Nsanganiyumwami na Waziri wa Fedha, Bajeti na Mipango ya Uchumi Dkt. Domitien Ndihokubwayo, walisema kuwa Rais wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan na Rais wa Burundi Mhe. Jenerali Evariste Ndayishimiye, walikubaliana kuwa ushirikiano kati ya nchi hizo ujikite pia katika masuala ya kiuchumi, hivyo utekerezaji wa mradi huo ni hatua muhimu katika kufungua nchi hizo kiuchumi.

Imelezwa kuwa reli hiyo itasaidia kusafirisha takribani tani zaidi ya milioni moja na madini zaidi ya tani milioni tatu kutoka Burundi kupitia reli hiyo na pia itasaidia kupunguza gharama za usafirishaji na kuchochea ukuaji wa viwanda, kilimo na uchumi kwa ujumla.

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.