MTANGAZAJI

WIZARA YA MALI ASILI NA UTALII KUTUMIA MFUMO WA KIELEKITRONIKI KWA WAGENI WA NDANI NA NJE YA TANZANIA

 

Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Utalii, Philip Chitaunga akizungumza na Wadau wa Utalii wanaotoa huduma za malazi kwa Wageni katika mikoa ya Dar es Salaam na Pwani  wakati wa   mafunzo ya usajili wa Wageni wanaolala kwenye huduma za malazi  kupitia   mfumo wa MNRT PORTAL yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam.

Watumishi wa Idara ya Utalii wakiwa tayari kwa ajili ya kuwahudumia Wamiliki wa Huduma za Malazi mara baada ya kumalizika kwa mafunzo ya usajili wa wageni wanaolala kwenye huduma hizo kupitia mfumo wa MNRT PORTAL.

Baadhi ya Wamiliki wa Huduma za malazi wakifuatailia mafunzo ya usajili wa Wageni kwenye mfumo wa MNRT PORTAL

Wageni wa ndani na nje ya Tanzania watakaolala  kwenye Huduma za Malazi zilizosajiliwa  na Wizara ya Maliasili na Utalii kwa mujibu wa sheria kuanzia Oktoba 1, 2020 watatakiwa kuanza  kusajiliwa kwenye mfumo wa kielekitroniki wa MNRT PORTAL.

Wageni hao watatakiwa kuwa na  Vitambulisho vya Taifa( NIDA) au Hati za Kusafiria na wale ambao hawatakuwa na vitambulisho hivyo  watasajiliwa kupitia namba za simu au Vitambulisho vya Udereva 

Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Utalii, Philip Chitaunga ametoa taarifa hiyo jijini Dar es salaam wakati alipokuwa akifungua mafunzo ya siku moja  ya Usajili Wageni wanaolala kwenye Huduma za Malazi kupitia  mfumo wa kielektoniki wa MNRT PORTAL  kwa Wamiliki wa Malazi wapatao 200 wa Kanda ya  Pwani.

Amesema lengo kuu la kusajili Wageni hao katika huduma hizo  ni kupata taarifa zitakazosaidia Serikali kupata takwimu sahihi kwa ajili ya  kuboresha sekta ya Utalii nchini.

Amesema taarifa hizo zitatumika kama nyezo katika kuandaa sera,mikakati na mbinu  katika kuboresha sekta ya utalii hasa utalii wa ndani ambao mwamko wake umekuwa mdogo kwa Wananchi

Mfumo  huo wa kusajili wageni utatumika katika Hoteli, Kambi pamoja na Loji pekee  zinazotambulika na Wizara hiyo

Amesema utaratibu huo wa kusajili Wageni  ni takwa la kisheria, Hivyo amewataka Wamiliki wa Malazi hao kuhakikisha kuanzia tarehe 1, Oktoba mwaka huu wanaanza kutekeleza agizo hilo kwa kusajili Wageni wanaofika katika Huduma za malazi kwa kutumia vitambulisho hivyo.

Katika hatua nyingine, Kaimu Mkurugenzi, Chitaunga amewatoa hofu Wamiliki wa malazi kuwa taarifa hizo  za Wageni zitatumika kwa ajili ya matumizi ya serikali pekee na zitatunzwa kwa usiri wa hali ya juu.

Kwa upande wake, Samson Nelsa ambaye ni mmiliki wa Huduma za Malazi katika mkoa wa Pwani, amesema mfumo huo utasaidia serikali kuandaa takwimu za idadi ya watalii 

Amesema mfumo huo mbali ya kuisaidia Serikali kupata takwimu za utalii wa ndani na wa nje pia utasaidia Wamiliki wa Hoteli kuwa na sehemu salama ya kuhifadhia taarifa zao.

Naye Mohamed Juma ambaye ni mmiliki wa Hoteli ya Rainbow licha ya kuipongeza Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kutaka kuwa na takwimu halisi za watalii kupitia mfumo huo utakaoanza kutumika mwezi ujao ameitaka Wizara hiyo kuwa  ihakikishe hakuna taarifa za wateja wao zinatumika kwa ajili ya maslahi binafsi

Pia Ameitahadhalisha Wizara kuwa makini katika kuulinda mfumo huo ili usiweze kudukuliwa na baadhi ya watu kwa ajili ya  maslahi yao binafsi.


No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.