MTANGAZAJI

MWINYI ASEMA KILA MTU ANAHAKI YA KUCHINJA KUTOKANA NA IMANI YAKE

Rais mstaafu wa awamu ya pili nchini Tanzania,Alhaji Ally Hassan Mwinyi amesema kila mtu ana haki ya kuchinja kutokana na imani yake ilimradi tu asivunje sheria za nchi .

Alisema anashangaa watu kugombania kitu kidogo kama cha kuchinja ilihali Tanzania ni nchi yenye  utamaduni wa kuwa na amani siku zote na kwamba kila mtu ana imani yake ya dini anayoiamini.

Hayo aliyasema jana katika hoteli ya Kilimanjaro wakati wa kongamano  juu ya utamaduni wa kiislamu Afrika Mashariki        ambapo Tanzania imechaguliwa kuwa mwenyeji wa kongamano hilo .

 “Imani ni nafsi ya mtu na haitakiwi mtu kumlazimisha kula nyama iliyochinjwa na mwenzio na kama unaona aliyochinja mwenzio ni kibudu basi usile chinja yako kula hata ukitaka kula  chura, mjusi konokono kula utakacho ruksa ilimradi tu usiingie katika jinai,”alisema Alhaji Mwinyi.

Pia alisema majaribu kama hayo yaliwahi kumtokea  wakati wa utawala wake lakini alijitahidi kuweka sawa kwa kumwambia kila mtu ale kile anachofikiri ni chakula bila kumlazimisha mwenzake ale anachokitaka yeye.

Alisema watanzania wamezaliwa ardhi moja na kwamba kinachotakiwa ni kuwa na misingi ya kuvumiliana na kwamba sifa ya uislamu ni pamoja na kuwa na uvumilivu si kufanya vurugu kama inayotafsiriwa na makundi ya wanaotaka kuvunja amani ya nchi kwa kutumia jina la dini ya kiislamu.

Pia alimshukuru Katibu Mkuu wa Shirikisho la Ulimwengu wa Kiislamu Duniani (RABITA) Dk.Abdullah Mohsin Al-Turki  kwa kuichagua Tanzania katika kuhubiri amani pia.

Naye Waziri wa maji Profesa Jumanne Maghembe ambaye alimwakilisha Makamu wa Rais Dk. Gharib Bilal amesema utamaduni wa kiislamu wa Afrika Mashariki na duniani kwa ujumla ni kuvumiliana katika dini huku akitolea mfano wakati wa kumaliza kuswali ndio maana mtu anageuza shingo huku na kule.

Pia aliwataka waislamu kujiendeleza katika elimu huku akieleza kuwa hata mtume alihamasisha hayo lakini waislamu wameshindwa kuyafuata.

Akitolea mfano alisema waislamu wanachuo kimoja kikuu huku dhehebu moja la Lutherani wanavyuo vikuu 11 hivyo ni vyema wakaungana na kujenga vyuo kwa ajili ya kusaidia kuongeza wasomi kutoka katika taaluma mbalimbali.

“Suala la elimu ya Dunia pia ni muhimu lakini mfano mzuri wa elimu kushuka ni katika mikoa ya pwani ambapo ndio ilipoanzia mwaka 1995 wanafunzi walioanza darasa la kwanza walikuwa 35,000 lakini walikuja kumaliza darasa la saba 9000 hapa inaonesha kua waislamu tunarudi nyuma badala kwenda mbele,”alisema Profesa Maghembe.

Hata hivyo alisema kua suala la kuporomoka kwa elimu wakati mwingine wa kulaumiwa ni wazazi kwa kushindwa kuwasimamia watoto wao katika maadili ya taaluma na wazazi kushindwa kuwasimaia katika misingi ya dini zote.

Dk.Abdullah Mohsin Al-Turki alisema katika nchi ya Saudia wanaishi watu tofauti tofauti lakini wakiwa katika upendo huku akisisitiza kikubwa ni kuheshimiana tu.

Alisema RABITA imekuwa ikifanya kazi katika nchi mbalimbali za Nigeria,Gabon,Jamhuri ya Kongo na baada ya ziara yake nchini hapa atahitimisha kwa kuitembelea Sudan.

Kongamano la RABITA limeandaliwa na Taasisi ya Masheikh na Wanazuoni wa Kiislamu Nchini ikiwa na lengo la kusisitiza amani nchini ambapo Alhaji Mwinyi ndio mlezi wao.

 

No comments

Mtazamo News . Powered by Blogger.